Simulizi la Shoga, Kijana Mweusi Aishiye Nje Kidogo ya Mji wa São Paulo, Aliyekuja kuwa Mtengeneza Filamu

Valter Rege akiwa kwenye paa la nyumba yao alikokuwa akitengeneza video kwa ajili ya idhaa yake ya mtandao wa YouTube iitwayo “Energia Positiva.” Picha: Vagner Vital/Agência Mural, imechapishwa kwa ruhusa yake.

Makala haya yaliyoandikwa na Vagner Vital yalichapishwa awali na Agência Mural. Yamechapishwa hapa kama sehemu ya kushirikishana maudhui kati ya Global Voices na Agência Mural. 

Akiwa na umri wa miaka sita, Valter Rege alitambua kuwa maisha yake yasingekuwa rahisi. Katikati ya matusi ya nguoni kama vile “nyani” na “basha,”  alipoteza meno yake alipoanguka  na kupigiza mdomo wake juu ya ukuta wa sehemu ya waenda kwa miguu shauri ya kusukumwa na wavulana wenzake. Alifahamu kwamba kuwa shoga na akabaki hai ingekuwa changamoto kwake, ingawa hakuwa na uwezo wa kusema maana ya neno hilo  [shoga] lililotumiwa na watu badala ya lake halisi wakati akifukuzwa na kupigwa.

Akihukumiwa kwa vile alivyokuwa, Valter Rege aligundua namna yake ya kupambana na unyanyapaa huo kwa kuongea kupitia kamera yake. Alitengeneza idhaa yake kwenye mtandao wa YouTube iliyokwenda kwa jina “Energia Positiva”  yaani (Nguvu Chanya) – kauli mbiu ambayo ilionekana kama tatoo kwenye mkono wake wa kulia pia– mahali ambapo hujadili, pamoja na masuala mengine, uwezweshaji wa watu weusi. Darini anakotengenezea filamu zake ni moja wapo kati ya makazi ya watu masikini yaitwayo Vila Clara, kusini mwa São Paulo,ambapo anamiliki studio yake ya nje.

Mahali pa kufulia pembeni ya matanki mawili ya kuhifadhia maji ni ushahidi kuwa sehemu hiyo ina matumizi mengine zaidi ya studio. “Sioni aibu kutengenezea video zangu hapa juu na kuonyesha mahali ambapo napaita nyumbani. Huu ndio ukweli wangu” alisema. “Mapaa haya unayoyaona ndio mitaa [ya nje ya mji].”

Akiwa na umri wa miaka takribani miaka 32, mwenye urefu wa mita 1.62 (zipatazo futi 5 , inchi 4) huku akiwa na tabasamu kubwa, hugawanya muda wake kati ya kutengeneza idhaa yake mtandao wa YouTube na kutimiza ndoto yake nyingine. Akisaidiwa na wafanyakazi wenzake, ameandika muswada uliompatia ruzuku kutoka Wizara ya Utamaduni huko nchini Brazili kwa lengo la kuzalisha filamu fupi iitwayo “Preto no Branco” yaani (Nyeusi juu ya Nyeupe). Filamu hiyo ambayo hata hivyo haijafahamika tarehe ya uzinduzi bado, inatarajiwa kuinua umaarufu wa Rege kikazi.

Picha ya filamu hiyo iitwayo “Preto no Branco.” Picha imechapishwa kwa ruhusa.

Filamu hiyo ni simulizi la kijana mmoja mdogo mweusi (ilichezwa na muigizaji Marcos Oliveira) ambaye anatuhumiwa kwa kosa la wizi baada ya kugongana na mwanamke mmoja mbele ya duka. Baada ya kupelekwa kituo cha polisi, na kufahamika hana hatia, maswali mengi yaliibuka ikiwa chanzo cha kukamatwa kwake kwaweza kuwa ni na chuki na ubaguzi wa rangi.

Sambamba na tukio hilo, Rege alisimamishwa na mwanamke mmoja ambaye alipiga kelele za mwizi alipokua akishuka kutoka kwenye basi kuelekea kazini: “Mwizi! Wewe ni mwizi! Umeiba simu yangu!” Katika hali ya mshangao na kuchanganyikiwa, akamjibu mimi sio mwizi huku akitembea kuelekea jengo alilokuwa akifanya kazi.

“Nilitamani kumwangali machoni nimwambie  hapaswi kutuhumu watu kwa namna ile, ila niliogopa. Niliogopa kupigwa na watu au askari ambao wasingenitendea haki,” anasema. Mwanamke yule aliwaita polisi, ambao baada ya muda mfupi waligonga mlango kwenye jengo la kampuni anayokuwa akifanya kazi. Kwa bahati nzuri, mlinzi wa kampuni hakuweza kuoanisha maelezo ya polisi na mtuhumiwa anayetafutwa ambaye alikuwa ni Rege, hivyo basi askari na mwanamke yule wote waliondoka.

“Kilikuja kikundi cha wanamgambo baada ya hapo. Nilikuwa na hofu ya kuwa mtu mwingine tena anaweza kuja kwa ajili yangu,” anasema. “Inasikitisha sana pale ambapo ulipitia nyakati kama hizi ukiwa mtoto na ukagundua kuwa nyakati zile zinaendelea kujirudia kwako hata ukiwa mtu mzima.”

1 maoni

jiunge na Mazungumzo

Mwandishi, tafadhali jiandikishe »

Miongozo

  • Tafadhali wape heshima watumiaji wengine. Maoni yenye lugha ya chuki, matusi na mashambulizi binafsi hayataruhusiwa.