Kwa nini Kiswahili hakijawa lugha inayounganisha Afrika?

Misemo katika lugha ya Kiswahili . Photo Credit; ultraBobban Attribution-Non Commercial 2.0 Generic (CC BY-NC 2.0)

Misemo katika lugha ya Kiswahili . Photo Credit; ultraBobban Attribution-Non Commercial 2.0 Generic (CC BY-NC 2.0)

JULAI 7 ilikuwa siku kubwa kwa Afrika iliposherehekea kwa mara ya kwanza Siku ya Lugha ya Kiswahili Duniani. Wananchi kote Kenya, Tanzania, Zanzibar, Afrika Kusini, na ulimwenguni waliadhimisha siku kwa kusherehekea barabarani na mitandaoni  kwa kutumia heshtegi #KiswahiliDay2022 na #KiswahiliDay. Hii ilikuwa siku ya kwanza rasmi tangu UNESCO ilipotenga Julai 7 kama siku ya lugha ya Kiswahili kuadhimishwa kote duniani mnamo November 2021.

Sherehe za maadhimisho

Tume ya Kiswahili Afrika (KAKAMA), shirika lisilo la kiserikali ambalo linahimiza na kuratibu ustawi wa Kiswahili, lilipatiwa fursa ya kwanza fursa ya kwanza kupanga matukio ya kuadhimisha siku kote Afrika Mashariki. Waandalizi waliandaa hafla katika makao makuu ya KAKAMA yaliyovutia wanachama kadha wa mataifa shirika katika Jumuia ya Afrika Mashariki.

Wakenya pia walitembea katika barabara za Jiji Kuu la Nairobi kuadhimisha sherehe hizo kwenye msafara ulioongozwa na Waziri wa Utalii nchini na Mkuu wa Kamati Simamizi ya Kitaifa ya Siku ya Kiswahili Duniani 2022, Najib Balala. 

Nchini Uganda, baraza la mawaziri liliidhinisha hoja kutumia Kiswahili kama lugha rasmi kufuatia uamuzi wa Februari mwaka uliopita wakati wa kongamano la 21 la Jumuia ya Afrika Mashariki (EAC), ambapo waliafikiana kutumia Kiingereza, Kifaransa na Kiswahili kama lugha rasmi za jumuia hiyo. Baraza la mawaziri Uganda pia lilipendekeza  shule za msingi na sekondari kufundisha Kiswahili darasani. EAC ni jumuia ya kieneo inayojumuisha nchi saba wanachama:  Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo,  mataifa ya Burundi, Kenya, Rwanda, Sudan Kusini, Uganda, Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, makao yake makuu yakiwa Arusha, Tanzania. Kiswahili ni lugha rasmi katika nchi zote sita washirika wa Uganda.

Nchini Tanzania, serikali ilitangaza mipango ya kujenga Chuo Kikuu cha Kiswahili na imetenga ekari 100 maeneo ya Pwani ya Bagamoyo kwa ujenzi wa mradi huo.

Mtandaoni, video iliyomjumuisha kiongozi wa upinzani Afrika Kusini  Julius Malema akizungumzia umuhimu wa kufundisha na kujifunza Kiswahili kama lugha ya kimataifa na kuhimiza Waafrika kukikumbatia Kiswahili kama lugha ya Afrika, iliibua hisia mseto kutoka kwa wananchi kote Afrika na kufufua mdahalo ambao unaendelea miongoni mwa wajuzi wa lugha na watetezi wa tamaduni: Kiswahili kinaweza kuwa lugha kuu ya Afrika?

Kiswahili: Miongoni mwa lugha 100 zinazofahamika zaidi 

Kikiwa kinatambuliwa kuwa miongoni mwa lugha 10 zinazozungumzwa zaidi duniani, na wazungumzaji zaidi ya 200 milioni, ndiyo lugha ya kwanza ya Afrika kupokea sifa za aina hiyo.

Tangu kuwa lugha kuu Afrika Mashariki, wazungumzaji wake sasa wameenea kwa zaidi ya nchi 14, ambazo ni pamoja na Zambia, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Malawi, Sudan Kusini, Msumbiji, Yemen, Oman, Somalia, na Comoros. Kiswahili kinafundishwa katika zaidi ya taasisi 100 Marekani pekee  pamoja na Uingereza,na Australia, kutaja tu baadhi yake.

Mnamo  2o2o, Afrika Kusini ilikuwa nchi ya kwanza kusini mwa eneo la Afrika kufunza Kiswahili kama somo la hiari shuleni. Mnamo Februari mwaka huu, Chuo Kikuu cha Addis Ababa nchini Ethiopia kilitangaza kwamba kitaanza kufundisha lugha ya Kiswahili.

Hata ingawaje Kiswahili kimekuwa lugha ya kwanza ya Kiafrika kutambuliwa rasmi, bado kuna mizimwi ya siku za nyuma.

Lugha ya fujo Uganda

Hatua ya baraza la mawaziri la Uganda kuidhinisha Kiswahili kama lugha rasmi  na mapendekezo kuwa kiwe lazima katika shule za msingi na sekondari hayakupokewa vyema na raia wa Uganda, ambao wana historia ngumu na  lugha hiyo. Kwa njia nyingine, kinaonyesha mapito ya nchi hiyo pamoja na ukandamizaji wa ulimwengu wa sasa. Wakati wa utawala wa  Idi Amin kutoka 1971–1979, kilifanywa lugha rasmi ya jeshi.

Kiswahili kilikuja kuonekana kama lugha ya fujo kwa sababu kilikuwa lugha rasmi ya jeshi na kuzungumzwa na wanajeshi. Pia Kiswahili kilisambaratika baada ya udikteta wa Amin kuangamizwa, na ni hadi miaka ya 1990 wakati wa kufufua Jumuia ya Afrika Mashariki na sera mpya ya National Resistance Movement language policy ambapo kiliweza angalau kurejesha kidogo umuhimu wake katika jamii ya Uganda.

Mazungumzo kuhusu utumizi wa Kiswahili na nafasi yake katika jamii ya Uganda yameendelea kushika kasi tangu kilipotangazwa kuwa lugha rasmi ya Jumuia ya Afrika Mashariki. 

Hata hivyo, hitaji la Kiswahili kwa misingi ya kiuchumi Uganda, ikiunganishwa na ongezeko la mtagusano wa kitamaduni katika Afrika Mashariki kupitia muziki, uhamiaji, pamoja na nia njema kisiasa, inaonyesha kuwa lugha hiyo haifai tena kukataliwa.


Lakini ni mapema kujua iwapo shinikizo la kitaifa kukumbatia Kiswahili kwa kukifanya somo la lazima shuleni litabadilisha mtazamo wa raia wa Uganda na kuwasaidia kukubali yaliyofanyika awali.

Tishio kwa lugha nyingine za Kiafrika

Kuenea kwa Kiswahili kote Afrika kumechukuliwa na baadhi ya wataalam wa lugha na watetezi wa lugha za Kiafrika kama tishio kwa lugha nyingine za Kiafrika. Tanzania, kwa mfano,ina sera ya lugha zenye ubaguzi discriminatory language policy  ambayo inaidhinisha utumizi wa Kiswahili katika wilaya za mashambani ambapo hakuna ufahamu au kuwepo kwa ufahamu mdogo wa lugha hiyo.

Hali hii ya kukipatia Kiswahili kipaumbele, bila kujali lugha za eneo, huathiri uwezo wa wanafunzi kuelewa masomo yao, na hatimaye kuwa na  athari zisizofaa kwa jamii  ambapo lugha kuu si Kiswahili.

Hatari kama hiyo ipo kwa sababu juhudi za kukuza Kiswahili hazilinganishwi na majaribio ya kuhimiza lugha nyingine.

Uundaji wa teknolojia ya lugha ya Kiswahili  

Kwa lugha zote za Kiafrika katika Jangwa la Sahara, Kiswahili ndicho kinaonekana zaidi mtandaoni. Hata ingawaje juhudi za kuunda teknolojia  ya lugha kwa Kiswahili zimekuwa taratibu, hili limekuwa lkikibadilika.

Mwezi huu, Meta ilichapisha utafiti  unaoelezea kwa kina jinsi wanavyopanga kufuatilia lugha 55 za Afrika zilizotengwa kwa lengo la kuimarisha maelezo yake yanayotafsiriwa kupitia kwa teknolojia zake katika majukwaa ya kijamii.

Abantu AI, kampuni ya Kenya, imeunda teknolojia ya mafunzo ya kina ya lugha za kiasili ambayo inatafsiri kutoka kwa lugha kubwa duniani hadi kwa lugha za kiasili za Kiafrika.

Kwa wakati huu, mfumo huo wa mafunzo unatafsiri kutoka kwa lugha kuu za kimataifa hadi kwa Kiswahili na lugha nyingine ya jamii moja nchini Kenya, ya Kikuyu. Teknolojia hiyo ya AI ambayo kwa sasa inaendesha harakati za kutafsiri lugha nyingi za Kiasili za Kiafrika, itaanza kutoa huduma zake kwa nchi nyingine za Afrika kufikia mwisho wa mwaka.

Zaidi ya hayo, Nanjala Nyabola, Msomi kutoka Kenya, mdadisi wa kisiasa, na Mkurugenzi wa  Global Voices’ Advocacy, amewezesha watu wanaozungumza Kiswahili kuongea na kutetea haki zao za kidijitali. Kwa ushirikiano wa kundi la wataalam wa Kiswahili, walitafsiri maneno yanayotumika katika teknolojia na haki za kidijitali hadi kwa lugha za Kiafrika zinazozungumzwa zaidi na kuunda kadi 52 muhimu ambazo zinaweza kudondolewa bila malipo free to download.

Kwa nini Kiswahili si lugha kuu ya Afrika?

Hata ingawaje nchi hizo zote zimeonyesha kujitolea kwao kuendeleza Kiswahili, kuna baadhi ya vikwazo vinavyoathiri ufanisi wake.

Kwa mfano, tofauti za kisiasa na kimaeneo Afrika, kama mataifa ya kaskazini kwa kuegemea Mashariki ya Kati badala ya mataifa mengine Afrika, huenda ikawa kikwazo kwa Kiswahili kuwa lugha inayozileta pamoja.

Ushawishi wa kigeni pia huenda ukatatiza “kukubalika” kwa Kiswahili. Afrika kwa sasa inategemea pakubwa China kwa msaada wa kifedha. Na kwa upande wake, China inatumia nafasi hiyo, kupenyeza lugha ya Mandarin katika nchi nyingi za Afrika, ambazo ni pamoja na Kenya. Katika baadhi ya maeneo, hili huenda likamaanisha kuwa Waafrika wanaweza kuzungumza Mandarin kwa ufasaha zaidi kushinda lugha zao za kiasili.

Mnamo 2018, kiongozi wa upinzani wa Afrika Kusini  Julius Sello Malema alishinikiza Waafrika kukubali, Kiswahili kama lugha ya Afrika  akidai kuwa serikali za Afrika ambazo zimeanza kutumia Mandarin bila kujali lugha za Kiafrika “zimekosea cha kupatia kipaumbele” 

 

Anza mazungumzo

Mwandishi, tafadhali jiandikishe »

Miongozo

  • Tafadhali wape heshima watumiaji wengine. Maoni yenye lugha ya chuki, matusi na mashambulizi binafsi hayataruhusiwa.