- Global Voices in Swahili - https://sw.globalvoices.org -

Je, Felix Tshisekedi Atamaliza Machafuko Katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo?

Mada za Habari: Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Haki za Binadamu, Siasa, Uandishi wa Habari za Kiraia, Utawala

Picha iliyopigwa kutoka kwenye TV5Monde ikionesha (kutoka kulia) wagombea katika uchaguzi mkuu 2018 wakijadili Felix Tshisekedi (Katikati) na Joseph Kabila (kushoto). Kupitia YouTube [1].

Mwezi Januari mahakama ya Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo ilimtangaza Felix Tshisekedi kuwa ni Rais mteule mpya wa Congo, ikitupilia mbali shauri lililofunguliwa na mshindi wa pili Martin Fayulu ambaye alidai kulikuwepo ulaghai katika kura.

Mwishoni mwa mwezi Disemba mwaka jana Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ilikuwa na uchaguzi mkuu uliokuwa na upinzani mkubwa baada ya Rais wa wakati huo Joseph Kabila kuitawala Kongo kwa miaka 18 na kukosa sifa kikatiba ya kugombea nafasi ya urais kwa kipindi cha tatu.

Uchaguzi huo ulitabiriwa kuwa wa kwanza wa “kubadilishana madaraka kidemokrasia kwa miaka 59 tangu Kongo ipate uhuru, [2]lakini uchaguzi huo ulighubikwa na mabishano tangu siku ya kupiga kura tarehe 30 Disemba.”

Mgombea aliyetegemewa kuibuka na ushindi Martin Fayulu wa chama cha uzalendo na Maendeleo alishtaki mahakamani akidai kura zake ziliibiwa. Yeye na wanachama wake waliamini ni mpango uliofanywa kati ya Tshisekedi wa chama cha Umoja wa Demokrasia na Maendeleo ya wananchi, [3] au UDSP na Rais Joseph Kabila wa chama kinachotawala cha Umoja wa Wakongo au FCC.

Tarehe 19 Januari 2019, Mahakama ilitupilia mbali madai ya Fayulu [4]kwa kushindwa kuthibitisha madai yake bila kutia shaka.

Kutokana na Tume Huru ya Uchaguzi, Tshisekedi alipata asilimia 38.5 [5] ya kura wakati Martin Fayulu wa umoja wa vyama vya upinzani Lamuka, alipata asilimia 34.7 na “Mwaminifu ” Emmanuel Ramazani Shadary alivuna asilimia 23.8. Mahudhurio ya wapiga kura yalikuwa ni asilimia 47.6 chini ya nusu ya wapiga kura wote.

Baada ya kutangazwa, shangwe za sherehe zilianzia makao makuu ya chama katika mji mkuu Kinshasa. Miongoni mwa marais wa nchi za Afrika; Rais wa Afrika ya Kusini Cyrill Ramaphosa alimpongeza Tshisekedi [6] na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania John Magufuli alituma ujumbe wake wa kumpongeza kupitia twiita.

Ingawa kulikuwa na kutokukubaliana na matokeo ya uchaguzi miongoni mwa wanachama wa Umoja wa Afrika, Umoja huo (AU) umempongeza na kumkaribisha Tshisekedi ambaye alitoa hotuba yake ya kwanza kwa umoja huo tarehe 10 Februari kushukuru ukaribisho.

Lakini miezi miwili baada ya uchaguzi huo wa mgogoro, wengi wanahofia kwamba kubadilishana madaraka kulifanywa kwa umakini kuhakikisha kwamba Kabila anaendelea kuwa madarakani [8] kupitia makubaliano aliyoyafanya na Tshisekedi.

Tshisekedi ni nani?

Félix Antoine Tshilombo Tshisekedi [11] alizaliwa Léopoldville tarehe 13 Juni, 1963. Baba yake ni Etienne Tshisekedi, ambaye alitawala sana siasa za Kongo kama mwanzilishi wa chama cha UDPS — ambacho ni chama kikubwa cha upinzani.

Kutokana na siasa za upinzani za baba yake, familia uliwekwa uhamishoni kwa nguvu [12] katika mji walimokuwa wanaishi wa Kasai miaka ya 1980. Baadaye Tshisekedi alisafiri na baba yake kuelekea Ubelgiji , ambapo alihitimu stashahda ya uhasibu mwaka 1987. Kati ya miaka ya 1991-2001 alipata shahada mbalimbali na kufanya kazi katika idara ya masoko.

Wakati yuko Ubelgiji aliingia kwenye siasa kama baba yake na akawa Katibu wa Taifa wa mahusiano ya Kimataifa wa chama cha UDPS mwaka 2008. Mwezi Novemba 2011, aligombea kuwa mwakilishi wa mji wa Mbuji Mayi katika Kasai lakini alikataa kutumikia nafasi yake akidai kulikuwa na udanganyifu katika uchaguzi.

Baba yake alitarajiwa kuchukua majukumu ya madaraka wakati Kabila akimaliza muda wake lakini kwa kifo chake kilichotokea tarehe 1 Februari, 2017, kijana wake Felix Tshisekedi alichaguliwa kuiongoza UDPS, akiaminiwa kuwa na uwezo wa kuongoza.

‘Askari wa watu’ — Maskitiko ya wapinzani yaendelea

Ushindi wa Tshisekedi unaweza kuleta amani katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo au kulipua machafuko kutegemea Fayulu, ambaye dhahiri aliyakataa [13] matokeo ya uchaguzi , kama atakubali au kukataa serikali hii ya mpito.

Fayulu aliyaita matokeo ya uchaguzi “Mapinduzi ya katiba” na “uchaguzi wa ghilibu.” Tarehe 14 Januari Kanisa la Romani Katoliki ambalo ni taasisi inayoheshimiwa sana katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, ilisema:

Matokeo ya uchaguzi wa Rais yaliyotangazwa na [tume ya uchaguzi] hayaendani na yale tuliyokusanya kwa kutumia waangalizi wetu.

“ Sio siri mmenichagua kuwa Rais,” Fayulu aliutangazia [14] umma, akijiona yeye kama Rais halali wa Jamhuri ya kidemokrasia ya Kongo. Fayulu amekuwa akihusika sana katika kampeni na amekuwa akiratibu na kuongoza maandamano ya kudai kuanzishwa kwa demeokrasia ya vyama vingi miaka ya 2016 na 2017.

Francesca Bomboko ambaye ni Mkurugenzi wa Berci International, kikundi cha utafiti na ushauri katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo aliimbia BBC kuwa Fayulu amehusika sana kumpinga Kabila. Fayulu amewaambia kwamba wakongo “wanamwita askari wa watu .” [15]

Fayulu alipochaguliwa kuwa mgombea wa vyama vya upinzani, Albert Moleka, mfanyakazi mwandamizi wa Etienne Tshisekedi, aliiambia BBC [15] kwamba Fayulu anaweza kuwa “Etienne Tshisekedi mpya,” akisema “ni yeye ambaye anafaa kuunganisha upinzani .”

Akiungwa mkono na makamu wa Rais wa zamani Jean-Pierre Bemba na Moise Katumbi, gavana wa zamani wa jimbo la Katanga lenye utajiri wa madini, Fayulu anaonekana kuwa na nguvu na ushawishi katika siasa za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Akiwa hana kuungwa mkono sana kutoka kwenye chama chake, ushindi wa Tshisekedi ulipatikana kwa mshangao. Kutokana na kikundi kinachohusika na migogoro kimataifa, UDSP iligawanyika katika makundi, baadhi walimkataa kumpa madaraka Tshisekedi ambaye ni mtoto wa Etienne.

Felix Tshisekedi pia ni mchanga sana katika nyanja hii ya siasa. Tshisekedi amekosolewa kwa kutojaliwa kipaji [16] na kutokuwa na uzoefu wa nafasi za juu katika kisiasa, anapata kuungwa mkono kisiasa kutokana na uwezo na sifa ya [17] baba yake, hii ni kutokana na Simon Allison wa Mail & Guardian.

Kwa upande mwingine, Tshisekedi ni “mwanadiplomasia, mtu wa maridhiano na msikivu wa watu,” alisema mwanachama wa chama cha upinzani cha Kongo [18].

Ameahidi kujenga nchi ya Amani, Utulivu na Umoja.

Tarehe 20 Januari Tshisekedi alisema kwamba ushindi wake kuthibitishwa na mahakama ni ushindi wa nchi nzima.

Ni Kongo iliyoshinda. Nimeingia kwenye kampeni ya kuwasuluhisha wakongo wote. Kongo haitagawanyika, wala haitakuwa ya chuki na ukabaila. Itakuwa Kongo yenye maelewano, Kongo yenye nguvu inayolenga Maendeleo, amani na utulivu.

Patrick Litanga, mwanafunzi wa Udaktari katika chuo kikuu cha Marekani katika mji wa Washington DC., akiwa anaongea na shirika la utangazaji la Al Jazeera, alisema [19] kwamba ushindi wa Tshisekedi unaweza kuwa mwanzo wa historia mpya ya siasa:

Felix Tshisekedi atakuwa Rais wa kwanza katika historia ya Kongo tangu kipindi cha Waziri Mkuu Patrice Lumumba kukabiliana na mihimili ya serikali yenye ukinzani mkali. Tunaweza kushuhudia mwanzo wa siasa za mihili ya dola kudhibitiana ili kuzuia matumizi mabaya ya madaraka.

Yajayo ya Jamhuri wa Kidemokrasia ya Kongo Yanakwazwa na historia yake mbaya

Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ilipata uhuru mwaka 1960. Tangu hapo, wananchi wamekuwa wahanga wa ukiukwaji wa haki za binadamu kama vile mauaji holela, mateso na ukiiukwaji wa kijinsia pamoja na ubakaji na utekaji. .

Mradi wa kukusanya taarifa ya migogoro Uppsala ilihitimisha kuwa serikali ya Laurent kabila ilishuhudia miaka mitatu yenye kiwango cha hali ya juu ya vifo vilivyosababishwa na migogoro, mwaka 1998 kulikuwa na vifo vipatavyo 13,884, mwaka 1999, vifo 8,019 na mwaka 2000 kulikuwa na vifo 7,537.

Je, serikali mpya ijayo ya Felix Tshisekedi itamaliza machafuko au itayachochea? Tusubiri.