- Global Voices in Swahili - https://sw.globalvoices.org -

Kutoka Mavumbini mpaka Ushujaa

Mada za Habari: Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara, Ulaya Magharibi, Mali, Ufaransa, Haki za Binadamu, Mahusiano ya Kimataifa, Uandishi wa Habari za Kiraia, Ubaguzi wa Rangi, Uhamiaji na Uhamaji, The Bridge

Mchoro umeandaliwa na mwandishi. Umetumiwa kwa ruhusa.

Nikiwa kama mtoto aliyesoma miandiko migumu katika lugha ya Kiarabu nchini Sudani, niliamini kuna watu wanaweza kuwa mashujaa. Lakini sikuelewa kwa nini hakuna mashujaa walioonekana kama mimi au hata kuwa na masimulizi ambayo watu kama mimi wangejitambulisha nayo. Labda hiyo ndiyo sababu niliamua kuwa mchora katuni?

Hisia zangu zote za utotoni zilinirudia jana kwenye mtandao wa Twita nilipokutana na video iliyokuwa inasambaa kwa kasi mtandaoni ikimwonesha mwanaume mmoja akikwea jengo lenye ghorofa nne kwa sekunde chini ya 20 ili amwokee mtoto, habari iliyopewa alama ishara ya #ParisSpiderman.

Wakati nikipitia habari mpya kwenye mtandao wa Twita, nikapata taarifa zaidi kuhusu utambulisho wa siri wa huyu jamaa wa #ParisSpiderman, ndipo maruriko ya habari yalipoanza. Jina lake ni Mamoudou Gassama na, alikuwa mhamiaji asiyeandikishwa kutoka Mali. “Huu ni mkakati mzuri zaidi -na wenye uhalisia zaidi kuliko Black Panther,” nilinong'oneza.

Nilipokuwa naendelea kutafuta taarifa zaidi kupata masimulizi ya shujaa huyu mpya, nilishangaa dini yake haikutajwa, kwa sababu hii ndiyo huwa sifa ya kwanza kutajwa kwenye vichwa vya habari wakati mhamiaji anapofanya kitu hasi.

Ndani ya saa kadhaa, vichwa vya habari viliripoti kuwa #ParisSpiderman amekaribishwa na rais wa Ufaransa na kwamba angepewa uraia. Utangulizi wa simulizi za kutoka mavumbini mpaka kuwa shujaa. Habari hazikuwa na undani wa kile hasa kilichotokea, isipokuwa maelezo ya kibaguzi (mweusi, masikini, anayehangaika na maisha, akiishi kwenye mageto), zikikimbilia kueleza kwa ufupi tukio la mtu huyu asiyefahamika akiokoa maisha ya mtoto -na PUU! -utangulizi wa shujaa mpya anayetoka kwenye jamii ya wachache, kipengele ambacho huongezwa kwenye masimulizi ya habari za mshujaa weupe.

Hapa ninakupa simulizi ambalo hatukusikia likizungumzwa: Gassama aliondoka Mali kama kijana kinda na alisafiri kupitia Burkina Faso, Libya -ambapo alikamatwa na kupigwa- hatimaye akaelekea ufukweni, alikopata usafiri wa maji kwenda Italia. Aliishi Italia kwa miaka minne kabla hajaelekea Ufaransa mwezi Septemba 2017 kuungana na kaka yake. Akiwa hana nyaraka za maana kumruhusu kukaa Ufaransa, alikuwa akilala sakafuni kwenye jengo la wahamiaji eneo la Montreuil, nje ya Paris, akiwa na kawaida ya kukunjua kigodoro chake kila usiku na kukufunga alfajiri. Alishirikiana chumba na wenzake sita na, kwa hakika, hakuweza kufanya kazi kwa mujibu wa sheria.

Kwa hiyo kupanda lile jengo ilikuwa ni moja wapo ya vitu rahisi zaidi Mamoudou kuwahi kuvifanya kwa miaka mingi.

Kile ambacho wasomaji wanahitaji kukielewa na kile ambacho wasimuliaji wanahitaji kukifanya wakati huu ni kuangazia kidogo zaidi undani wa maisha ya shujaa huyu na ugumu aliopambana nao kabla hajapanda ghorofa lile kumwokoa mtoto. Shujaa huyu, shujaa mkuu wa mashujaa, alikuwa mhamiaji lakini pia alikuwa na “moyo mwema”, moyo ambao unaonekana ‘wa kawaida” na hakuwahi kusumbuliwa mara kwa mara wala kufuatiliwa.

Hebu utambulisho wa shujaa huyu mpya na wa tofauti uifanye Ufaransa, na dunia yote, kutambua mashujaa wangapi wameingia kwenye nchi hiyo kwa kutumia boti na bado wanangoja kutambulisha ushujaa wao.

Suala jingine: Je, shujaa wetu huyu atamudu dakika tano za umaarufu? Atawezaje kuishi sasa ambapo nguvu zake zimegundulika?