- Global Voices in Swahili - https://sw.globalvoices.org -

‘Bustani’ Shirikishi Inayotumia Matangazo ya Radio Kukuwezesha Kuzuru Ulimwengu

Mada za Habari: Ulaya Magharibi, Uholanzi, Teknolojia, Uandishi wa Habari za Kiraia, Sauti Chipukizi

Makala ifuatayo imetafsiriwa na mwandishi wetu mpya, Samweli Kabulo, aliyeungana nasi hivi karibuni. Ikiwa unapenda kuungana nasi pia, karibu uwasiliane nasi.

Picha kificho ya Radio Garden, jukwaa la mtandaoni, ambalo tangu mwka 2016 limekuwa likiwawezesha watu kusikiliza radio mbalimbali kutoka sehemu tofauti ulimwenguni.

Kuna sauti za kila namna unazoweza kuzisikiliza duniani kote, na moja wapo ni mradi wa mtandaoni unaopatikana Uholanzi unaokuwezesha kufanya hivyo.

Tangu mwishoni mwa mwaka 2016, Radio Garden [1] imekuwa ikiwaunganisha wasikilizaji kwenye orodha ya vituo vya redio vinavyoongezeka kwa kasi kutoka sehemu mbalimbali ulimwenguni.

Usanifu wake ni wa kawaida sana kama unavyoonekana. Ni ramani shirikishi yenye vidoti vya kijani vinavyowakilisha miji mbalimbali. Ukibonyeza kwenye kidoti unakuwa umebonyeza kwenye mojawapo ya kituo kati ya vituo vya redio vilivyochaguliwa katika mji huo. Kwa bahati unaweza ukapata taarifa rasmi ya habari mpya kutoka redio Tonga. Ni redio ya zamani ya Iran inayoburudisha hadhira wakati wa masaa ya usiku ikiwa wamelala. Au unaweza kubahatika kusikiliza moja ya vituo vichache vya redio vinavyoendelea kujaza mawimbi ya sauti katika mji wa Siria wa Aleppo.

Bofya kwenye sehemu ya “Kumbukumbu” kwenye Radio garden ili upelekwe kwenye sehemu muhimu ya kumbukumbu ya matangazo ya radio ya nchi husika.

Sifa nyingine nzuri ya redio hii ni pamoja na uwepo wa kipengele cha mziki wa zamani na matangazo ya sauti ya kihistoria; Sehemu ya “sauti za asili” kama jina linavyotanabaisha, inakupa matangazo ya asili ya radio maarufu za jiji, na sehemu ya “simulizi” inayokupa maelezo ya moja kwa moja ya namna watu wanavyojihusisha na radio za jamii. Kwa mara nyingine haya yote yatakupeleka sehemu tofauti ulimwenguni, inaweza kuwa ni mji mkuu wa Taiwan wa Taipel au mji mkuu wa Australia, yaani Sydney.

Hii hapa ni video ya Youtube inayoielezea Radio Garden na namna inavyofanya kazi:

Mpango huu ulibuniwa na Taasisi ya Matangazo ya Sauti na Picha [2] ya nchini Uholanzi chini ya usimamizi wa Golo Föllmer wa Chuo Kikuu cha Martin Luther cha Halle-Wittenberg. Ubunifu huu ulizingatia utaalam wa makampuni mawili ya nchini humo ambayo ni Studio ya Puckey na Moniker, ambao walikubaliana kuwa namna nzuri ya kufanikisha kazi hii ilikuwa ni kuunda ramani iliyosheni isiyo na mipaka wala kuonesha majina ya miji.

Mara tu baada ya kuanzishwa rasmi kwa Radio garden, ilipata umaarufu mkubwa kweye mitandao ya kijamii. Mmoja wa wasanifu wake, Jonathan Puckey aliliambia The Guardian [3] kuwa alifurahishwa sana na majadiliano aliyoyashuhudia kuhusiana na mradi huu.

Kwenye mtandao wa Reddit, radio hii iliibua mjadala mzuri sana, ambapo watu waliongelea uzoefu wao walipokutana na radio, au mababu zao waliofanya kazi radioni wakati wa vita ya pili ya dunia.

Katika Ukurasa wa Facebook [4] wa mradi huu, kumekuwa pia na maoni ya kutia moyo sana na uungwaji mkono, kwani watumiaji kutoka maeneo mbalimbali wamekuwa wakiweka mapitio yenye kupongeza na kusifia.

Mbali na kuwepo kwa tovuti, Radio Garden ina kitumizi cha mfumo endeshi wa iOS [5] na wa fivaa vyaAndroid [6], hali inayowawezesha watumiaji wake kusikiliza matangazo ya radio kwa uhuru wao- hata kama simu janja zao zitakuwa kwenye hali ya kuzimika kiasi.