- Global Voices in Swahili - https://sw.globalvoices.org -

Mkimbizi na Mchora Vibonzo wa Korea Kaskazini Achora Kuhusu Maisha Yalivyo Kwa Watu Wanaotoroka

Mada za Habari: Asia Mashariki, Korea Kaskazini, Korea Kusini, Sanaa na Utamaduni, Uandishi wa Habari za Kiraia, Wakimbizi

Kushoto, mkimbizi mmoja akiuliza, “Una uhakika kuwa tutakula kwa kadri tunavyotaka?” Kulia, mkimbizi mwanamke mmoja anasema, “Vyakula vyote vya mgahawa huu vimeoza”. Wakorea Kusini hutumia neno la Kiingereza “makofi” na linaposikika hushabihiana na neno la Kikorea “kuoza.” Changamoto kubwa kwa wakimbizi wa Korea Kaskazini ni kujifunza maneno haya ya kigeni ambayo yamekuwa sehemu ya lugha ya asili ya Wakorea Kusini. Credit: Choi Seong-guk

Habari hii ya Jason Strother [1] ilichapishwa awali kwenye   [2]mtandao wa PRI.org [3] mnamo Julai 6, 2017. Imechapishwa tena kama sehemu ya makubaliano kati ya PRI na Global Voices.

Kutoroka kwa wakimbizi wapatao 30,000 kutoka Korea Kaskazini kwenda Korea Kusini haiwezi kuonekana kuwa habari kubwa ya kuchekesha. Lakini mtandao wa mfululizo wa vibonzo uliotengenezwa na mkimbizi wa Korea Kaskazini, ambaye sasa anaishi Seoul amejaribu kuleta ucheshi kidogo katika safari ambayo mara nyingi ni ya taabu na makazi mapya magumu.

Baada ya yeye mwenyewe kukimbilia Korea Kusini mwaka 2010, Choi Seong-guk, 37, aligundua kuwa Korea mbili hazikuwa tena nchi moja- tofauti nyingi za utamaduni na lugha zilikuwa zimeibuka katika kipindi cha zaidi ya miaka 70 ya mgawanyiko.

Kwa Choi, ambaye alishawahi kufanya kazi katika studio kubwa ya vibonzo huko Pyongyang, SEK, tofauti ya kwanza iliyojitokeza ni kuwa vibonzo kwa upande wa Kusini havikuwa chochote kwa vile vya upande wa Kaskazini.

“Kwa mara ya kwanza nilipoviona vibonzo vya Kusini, sikuvielewa,” alisema. “Hakuna hadithi kuhusu uzalendo, kukamata majasusi au vita. Vilionekana havina maana kwangu.”

Choi amekuwa na ujuzi wa kuchora tangu akiwa mdogo, wakati waalimu walipomsifia kwa michoro yake ya Askari Wabaya wa Marekani ambapo alisema aliwafanya ” wawe wabaya na wakatili kwa kadri alivyoweza.”

Haya ni marudio ya mchoro wa Choi aliouchora akiwa mwanafunzi. Inamuonesha askari wa Marekani akimpiga mateke askari wa Korea Kusini wakati wakijiandaa kuvuka mpaka kwenda Korea Kaskazini. Maelezo yanasomeka, “Uvamizi kutoka Korea Kusini” Shukrani: Choi Seong-guk

Mwaka 2016, Choi alirudi katika uchoraji na alianzisha mtandao wa mfululizo wa vibonzo ulioitwa “Rodong Shimmun,” ikiwa na maana ya “kuhojiwa kazi” — ni akilichezesha jina la “Rodong Shinmun,” ambalo ni gazeti la kazi la Korea Kaskazini.

Mfululizo wa mizaha ulifuatiwa na kundi la wakimbizi wapya waliofika karibuni ambao walitumia miezi yao ya mwanzo katika kituo cha mahojiano kinachoendeshwa na serikali ya Korea Kusini. Choi alichochea utani katika ‘upya wao’ kama vile mshangao wao katika aina za vyakula katika mgahawa.

Pia alihadithia kuhusu mkimbizi mmoja asiye na mapenzi, ambaye husema hiyo imetokana na aibu yake mwenyewe ya kutokuelewa utamaduni.

Mkimbizi anakutana na mwanamke mmoja wa Korea Kusini, ambaye anasema “amevutiwa”. Sijawahi kuonana na mtu wa Korea Kaskazini kabla. Je naweza kupata namba yako ya simu?” Credit: Choi Seong-guk

“Mara moja nilikutana na mwanamke wa Korea Kusini aliyetaka namba yangu ya simu na alisema angependa kuwa rafiki yangu” alikumbuka. “Nami nilitafsiri ndivyo sivyo kuwa anataka tuoane.”

Mwanamke aliendelea kutumia neno hilo la mapenzi ambalo hutumika kikawaida Korea kusini. Baadaye katika kisanduku cha maneno, Choi aliwaeleza wasomaji wake jinsi lilivyomsababishia mkanganyiko wa hisia au ishara.

“Katika Korea Kaskazini, ni watu walio katika mahusiano ya kimapenzi pekee wanaweza kuambiana hivyo” Baina ya marafiki huwa tunaitana ‘komredi.'”

Hata hivyo, Sio michoro yote ya Choi ni ya kuchekesha. Mingine huonesha watu wakifa njaa mitaani huko Korea Kaskazini.

Katika mifululizo yote ya vibonzo vya Choi inaoneshwa mitazamo ya maisha ya Korea Kaskazini. Katika mchoro huu mtu anasema ” Wewe, unaweza kufa. Tunaweza kula hizi nyasi.” Credit: Choi Seong-guk

Nyingine zinaonesha jinsi wakimbizi wanavyotoroka chini ya mtutu wa moto wa askari wa mpakani.

Choi anasema anatumaini kuwa mfululizo wa vibonzo vyake utasaidia kubadili mitazamo ya wa-Korea Kusini ambao hawahisi huruma dhidi ya wakimbizi kutoka Korea Kaskazini.

Maelezo juu ya mchoro yanasomeka: “Kutoroka Korea Kaskazini inahusu kuishi. Hata kama mmoja wa wanafamilia wako atapigwa risasi na kuanguka, utaendelea tu kukimbia” Credit: Choi Seong-guk

Na inaweza kuwa inafanya kazi.

“Rodong Shimmun” sasa inapokea makumi elfu ya watazamaji na baadhi ya wasomaji huacha maoni wakisema imewasaidia kuwa na uelewa mzuri juu ya utofauti wa utamaduni kati ya Korea Kusini na Korea Kaskazini. Wengine wanaandika kuwa sasa wanahisi huruma juu ya wakimbizi.