- Global Voices in Swahili - https://sw.globalvoices.org -

Maisha Ndani ya Kituo cha Kulelea Watu Wenye Ukoma Nchini Myanmar

Mada za Habari: Asia Mashariki, Myanmar (Burma), Afya, Safari, Uandishi wa Habari za Kiraia, Utawala
[1]

Makazi ya watu wenye ukoma, Mt. Yosefu Cotto Legnos kusini kwa jimbo la Shan. Picha ya Pyay Kyaw/The Irrawaddy

Makala [1] haya yaliyoandikwa na Pyay Kyaw yanatoka The Irrawaddy, tovuti huru ya habari nchini Myanmar, na yamechapishwa na Global Voices kama sehemu ya makubaliano ya kubadilishana maudhui.

Kikiwa maili saba kutoka mji wa Loilen kusini mwa jimbo la Shan, kituo cha kulelea watu wenye ukoma kiitwacho Mt. Yosefu Cotto Legnos— kinachofahamika pia kama makazi ya wenye ukoma Hohkai— kilianzishwa na padre wa ki-Italia zaidi ya miaka 70 iliyopita na sasa kinatunza watu 90 wenye ukoma wanaotoka kwenye maeneo mbalimbali nchini Myanmar.

Wagonjwa wana kati ya umri wa miaka 13 mpaka 80 na wengi wao wanasumbuliwa na kuharibika kwa miguu hali inayosababishwa na ugonjwa huo na wanaangaliwa na watawa.

Wale wanaoishi kwenye kituo hicho wanafanya kazi za shamba na kuangalia mifugo, lakini wanachozalisha kinaishia kwenye masoko ya jirani kwa sababu ya unyanyapaa.

Wengi wa wagonjwa hao hawana mpango wa kurudi kwa familia zao, lakini wamemwachia Mungu hatma yao.

Mmoja wa wagonjwa wa namna hiyo, akiitwa Maya, alisema ana mpango wa kufia kwenye kituo hicho. Alikumbuka namna alivyolazimishwa kuishi kwenye eneo la makaburi yaliyopo mjini kwao kwa sababu ya kuugua ukoma na wakati mwingine akiibia kuonana na familia yake nyakati za usiku.

Kituo hicho hakipokei fedha yoyote kutoka serikalini pamoja na msaada mkubwa inayoutoa kwa watu wanaoishi na ugonjwa huo na hivyo kutegemea misaada kutoka nchi nyingine.

Wagonjwa wa ukoma wasiotaka kuendelea kuishi kwenye kituo hicho, mapadre wameanzisha makazi maalum yenye vijiji vitano vyenye uwezo wa kuhifadhi watu 300.

Mwaka 2003, serikali ilitangaza kuwa imefanikiwa kukomesha ugonjwa huo kabla ya muda uliokadiriwa kufuatia kupungua wagonjwa mpaka kufikia mgonjwa mmoja katika watu 10,000.

Ingawa idadi ya wagonjwa wapya nchini Myanmar imepungua kwa miaka 10 iliyopita, kulikuwa na wagonjwa 2,877 mwaka 2014 na wagonjwa 2,571 mwaka 2015 kwa mujibu wa takwimu za Hospitali Kuu ya Rangoon.

Hapa chini ni baadhi ya picha zinazoonesha maisha ya kila siku ya watu wanaoishi kwenye makazi hayo ya watu wenye ukoma:

[1]

Kila siku saa 12 asubuhi, wagonjwa -wengi wakiwa dhaifu – hufanya sala kwenye kanisa lililopo kwenye makazi hayo. Picha na maelezo na Pyay Kyaw / The Irrawaddy

[1]

Wagonjwa wenye nguvu huwapikia wenzao walio dhaifu. Picha na maelezo na Pyay Kyaw / The Irrawaddy

[1]

Wale wanaoishi kwenye makazi hayo wanafanya shughuli za shamba na kuangalia mifugo, lakini wanachokizalisha kinabaki kwenye masoko ya jirani kwa sababu ya unyanyapaa dhidi ya wenye ugonjwa huo. Picha na maelezo Pyay Kyaw / The Irrawaddy

[1]

Kilimo kwenye makazi hayo. Picha na Pyay Kyaw / The Irrawaddy

[1]

Wale wanaoweza kufanya kazi kwenye mashamba na mapori wanarudi kituni saa za jioni na kupumzika. Picha na maelezo na Pyay Kyaw / The Irrawaddy

[1]

Kuoga kwenye makazi hayo. Picha na Pyay Kyaw / The Irrawaddy

[1]

Ratiba ya jioni kwenye makazi hayo. Picha na Pyay Kyaw / The Irrawaddy