Karibu Msumbiji, Ukutane na Serikali Inayofunga Kamera 450 Kukufuatilia
Dércio Tsandzana Liam Anderson Christian BwayaCensorship
Kwa mujibu wa moja wapo ya magazeti yanayoaminika zaidi nchini Msumbiji, Canal de Moçambique, serikali imeanza kufunga kamera 450 za usalama kwenye miji ya Maputo na Matola, kama sehemu ya mradi wa “Mpango wa Taifa wa Kufuatilia Habari”, ambao unadaiwa kuwa na mipango ya kufuatilia nyendo za wananchi wa kawaida. (Mapema mwaka huu mwezi Mei, Global Voices iliandika kuhusu mpango huu wa Msumbiji wenye utata.)
Kwa mujibu wa Canal de Moçambique, serikali imeingia mkataba na “Kampuni ya Uwekezaji ya Msumbiji” kufunga kamera hizo, bila ushindani wa zabuni. Kampuni hiyo, hata hivyo, inamilikiwa na mtoto wa Rais wa zamani Armando Guebuza, aliyetoa kazi hiyo kwa kampuni ya ki-China “ZTE” kufanya kazi hiyo, linasema gazeti.
Egídio Vaz, mchambuzi maarufu na mwanaharakati wa mitandaoni, alionesha wasiwasi wake kwa hali hiyo:
[…] Kwa zaidi ya miezi miwili, tumesoma habari za miradi mikubwa ya watoto wakubwa wa nchi hii. Nimejisikia vibaya. Hii si sahihi hata kidogo. Lakini kuna tiba ya hali hii kwangu. KUSAHAU.
Schauque Spirou alizungumzia uwezekano wa matokeo ya kufungwa kwa kamera hizo za usalama kwenye miji yote ya Maputo na Matola, akijaribu kukumbuka kile kilichotokea Brazil:
Tunaamka taratibu, au tunalala bila kujua…lakini hakuna mashaka kuwa Mkubwa yuko kazini…taarifa zilizoandikwa na Canal de Moçambique kuhusu kamera za usalama -nadhani zisichukuliwe kirahisi: isipokuwa “utoaji wa zabuni” wa namna hiyo…
Nchini Brazil, kuna mazungumzo ya “biashara ya kupiga faini”, kwa sababu kamera za usalama zilizofungwa kwenye mitaa ya São Paulo inatumika kuwamata “Madereva Formula 1 ”… lakini pesa zinazoingizwa kwa faini hizi zinasababisha hali ya kutokuaminika.
Kwa mujibu wa Canal de Moçambique, hata hivyo, serikali inaweza kuwa na uwezo wa kisheria kuingia mkataba na kampuni yoyote bila ushindani za kizabuni, kwa sababu sheria ya manunuzi ya nchi hiyo inaweka mwanya huo kwa masuala yanayohusu usalama wa taifa. Lakini bado, hata hivyo, sheria hiyo haihallaishi uamuzi huu wa kutoa tenda kwa mtoto wa Guebuza, kwa kuzingatia uwezekano wa mgongano wa maslahi.