- Global Voices in Swahili - https://sw.globalvoices.org -

Mfungo wa Radhamani Wawafanya Wakimbizi wa Kiislamu Nchini Uturuki Wakumbuke Nyumbani

Mada za Habari: Mashariki ya Kati na Afrika Kaskazini, Ulaya Magharibi, Syria, Ugiriki, Dini, Uandishi wa Habari za Kiraia, Wakimbizi
Renna Ramadan prepared an iftar meal for her family, Syrians from Idlib who hoped to reach Northern Europe but instead are living in the passenger waiting area at Piraeus Port Terminal 1 in Athens, Greece. Several hundred refugees and migrants remain at Piraeus, long after Greek authorities vowed to move the people to other camps. Credit: Jodi Hilton/Pulitzer Center

Renna Ramadan akiandaa futari kwa ajili ya familia yake, wa-Syria kutoka Idlib waliokuwa na matumaini ya kufikia Kaskazini mwa Ulaya lakini kinyume chake wamekuwa wakiishi katika eneo maalum kwa ajili ya abiria kusubiria katika bandari ya Piraeus huko Athens, ugiriki. Mamia mengine ya wakimbizi na wahamiaji wamesalia huko Piraeus, kwa muda mrefu baada ya mamlaka za Ugiriki kuapa kuwapeleka watu wengine katika kambi zingine. Picha: Jodi Hilton/Kituo cha Pulitzer

Makala haya ya Jeanne Carstensen [1] yalichapishwa awali kwenye tovuti ya PRI.org [2] mnamo Juni 10, 2016, na yanachapishwa kwa mara nyingine hapa kama sehemu ya makubaliano ya kushirikiana maudhui.

Katika usiku wa kwanza wa mfungo wa Ramadhan, wakazi wa kambi isiyo rasmi ya mahema katika bandari ya Piraeus jijini Athens walijipanga kwenye foleni kupokea futari ya kufuturia.

Wakati jua linapozama nyuma ya vivuko vingi vinavyosafirisha wasafiri kwenda katika visiwa vya Ugiriki, mamia ya wakimbizi waliochoka na  kutweta jasho jingi, wamepanga mstari mbele ya behewa kubwa lililowekwa katika viwanja vikubwa vya maegesho. Hawajala au kunywa maji tangu saa kumi alfajiri.

Ni wazi kuwa serikali ya Ugiriki inajaribu kuwasaidia wakimbizi hawa katika kipindi hiki cha mfungo wa Ramadhani. Pamoja na hivyo, hali ya hapa Piraeus inakatisha tamaa kabisa.

Hedda Grew, ambaye anajitolea pamoja na wanafanyakazi wa Asasi Isiyo ya Kiserikali ya Sweden, anasema kuwa; mfungo wa Ramadhani unaongeza kadhia kwa watu ambao tayari wana mfadhahiko mkubwa wa hali ya sasa. “Hawawezi kula, hawawezi kunywa chochote, yaani wamekaa tu ndani ya mahema yao yaliyo na joto kali kwa siku nzima; na huu ni mchanganyiko wa Ramadhani na kusubiri ”  ndivyo alisikika akisema.

Na kuna msururu wa kusubiri unaokera.

Ninatembea katika eneo lililo kimya katika kambi ambapo ninakutana na Amal Herh, ambaye ni mama wa watoto wanne  ni mrembo na kijana bado anayetokea Aleppo.

Jina lake linamaanisha “Tumaini” kwa Kiswahili. “Nina matumaini makubwa” alisema, “Lakini sasa lazima niwe jasiri na imara kwa ajili ya familia yangu”

Amal ana uso uliojaa bashasha, lakini hata hivyo unaweza kuona fadhaa katika macho yake. Ananiambia kuwa mfungo huu wa Ramadhani unamfanya akumbuke sana nyumbani.

“Nataka kwenda Aleppo kwa ajili ya Ramadhani, ambapo kuna mapishi ya kila aina na maji baridi na mahali pazuri pa kukaa, sio kama hivi”. Matunda mazuri ya aina tofauti na sio haya machungwa ya kila siku. Huwezi kula chakula hicho hicho kila siku ukakipenda, sivyo?” alisema Amal.

Nilimwambia kuwa ninamuelewa sana. Watu hao waliniambia kuwa Ramadhani ni kipindi cha furaha sana kwa mwaka ukiwa na familia yako huku mkishirikiana vyakula maalum.

“Ndio” alisema, “Ila siwezi kusema hili nilisemalo kwako kwa sasa kwa sababu nina huzuni sana, kwa sababu nimeikumbuka nyumba yangu”

Usiku uliofuata nilikubali mualiko wa kula futari iliyokuwa na utofauti kidogo na ile ya jana iliyokuwa nyumbani kwa Anna Stamou, mwanamke wa Kigiriki aliyebadili dini na kuwa Muislam, na mume wake Naim el Ghandour, Rais wa Jumuiya ya Kiislam huko Ugiriki. Naim alizaliwa Misri.

Picha katika simu yake kwa Ramadhani hii inaonesha ishara ya jua kuzama ikiwa na muito wa adhana. Katika meza kulikuwa na utani kuhusu saladi iliyoandaliwa kuwa ilikuwa ya Kimisri au ni ya Kigiriki?

Baada ya futari  Anna alimtafsiria Naim wakati akiongea Kigiriki. Anahuzunika kwa ajili ya maelfu ya wakimbizi wa Kiislamu wanaosherehekea Ramadhani ndani ya kambi. Lakini alisema kuwa anafarijika kuona Yannis Mouzalas, waziri wa Uhamiaji nchini Ugiriki akifanya jitihada za kuwasaidia wakimbizi hao wakati huu wa Ramadhani. “Inatutia moyo sana” alisema Naim.

Wakimbizi wapo katika hali mbaya sana hapa Ugiriki. Lakini Naim aliyekimbia asili yake ambayo ni Misri mwaka 1967, anashukuru kuwa wakimbizi hao angalau wako mbali na vurugu.

Aliendelea kusema kuwa; “hapa wako na unafuu zaidi kuliko wangekuwa kule na labda bomu lingeshawaangukia sasa hivi na wasingeweza kusherehekea Ramadhani, wala chochote.

Lakini baraka na zawadi bora kabisa kwa ajili ya Ramadhani ingekuwa kumaliza mapigano. “Natamani kungekuwa na suluhisho kwa Ulaya kumaliza vita” kwa sababu imeshakuwa ngumu kumaliza  hivyo vita. Wote wanataka kurudi nyumbani kwao. Tunawaombea kwa hakika kuwa Ramadhani ijayo itukute hatuna vita kati yetu.

Baadaye niliendelea kuwaza kuhusu Amal akiwa kule kwenye hema lake kule Piraeus. Sio rahisi kuuona utu wako ukipotea hivi hivi hasa katika kipindi cha mapumziko. Ninatamani ningeweza kumletea maji baridi na machungwa yaliyochumwa  na kumwenywa muda huo huo kutoka  Aleppo kwa ajili ya Ramadhan.

Jeanne Carstensen na Jodi Hilton wanaandika habari za janga la wakimbizi nchini Ugiriki kwa msaada wa kituo cha Pulitzer.