- Global Voices in Swahili - https://sw.globalvoices.org -

Raia wa Iraqi Aliyefanya Kazi ya Ufasiri kwa Jeshi la Marekani Akwama Ugiriki

Mada za Habari: Marekani ya Kaskazini, Mashariki ya Kati na Afrika Kaskazini, Ulaya Magharibi, Iraq, Marekani, Syria, Ugiriki, Uturuki, Uandishi wa Habari za Kiraia, Vita na Migogoro, Wakimbizi
Ibrahim Esmael Ibrahim at the train station in Idomeni, Greece. As a teenager, he worked as a translator with the US military in Iraq. Credit: Filip Warwick. Used with PRI's permission

Ibrahim Esmael Ibrahim akiwa kwenye kituo cha treni mjini Idomeni, Ugiriki. Akiwa kijana, alifanya kazi kama mfasiri wa wanajeshi wa Marekani nchini Iraq. Picha: Filip Warwick. Imetumiwa kwa idhini ya PRI

Makala haya yaliyoandikwa naJacob Resneck [1]  [2] awali yalionekana kwenye mtandao wa PRI.org [3] mnamo Machi 24, 2016, na yamechapishwa tena hapa kama sehemu ya makubaliano ya kubadilishana maudhui.

Ibrahim Esmael Ibrahim ana umri wa miaka 26, mtanashati anayetoka Baghdad.  Nilipokutana naye, alikuwa amesimama kwenye kibaraza cha kituo cha treni mjini Idomeni, Ugiriki — ingawa hapakuwa na treni inayopita wakati huo. Ibrahim anaongea Kiingereza kizuri; kabla hajafikisha miaka 20 alipata kazi kwenye kampuni iliyoko Viginia iitwayo GLS (Global Linguist Solutions [4]), iliyotoa wafasiri kwa ajili ya jeshi la Marekani wakati wa vita vya Iraq.

Anasema malipo yalikuwa mazuri — Dola za Marekani 1,500 kwa mwezi pamoja marupurupu. Wanajeshi walimpenda na wakampachika jina la utani AP. Lakini baada ya miezi sita ya kufanya kazi, Ibrahim anasema maisha yake yalihatarishwa na wanajeshi hao.

“Waliniambia nitakata kichwa chako na kukitenga na kiwiliwili kama nitakuona hapa tena,” anakumbuka.

Familia ya Ibrahim ilimsihi ahame nchi. Lakini kabla hajafanya hivyo, aliwandikia wanajeshi wa ki-Marekani waliokuwa rafiki zake kuwaambia kile kilichokuwa kinaendelea.

“Niliwaambia kilichonitokea na wakaniambia niwape GLS [shirika lililomwajiri] kitambulisho changu kwenye eneo ambalo halikuwa na mapigano mjini Baghdad,” anasema, akikumbuka tukio hilo miaka kumi baadae. “Kwa hiyo nilienda pale na kuwapa [kitambulisho] na kesho yake nikachukua basi kwenda Syria.”

Akiwa Damascus, alipata kazi ya ofisini kwenye kampuni ya simu. Lakini alikuwa na ndoto ya kwenda Marekani anakoishi dada yake. Shemeji yake alimwambia kwa kufanya kazi na Jeshi la Marekani nchini Iraq, angeweza kuomba Visa Maalum kwa Wahamiaji nchini Marekani.

Lakini ili kufanya hivyo, alihitaji ushahidi kuwa aliwahi kufanya kazi ya Ufasiri. Kwa hiyo akawaandikia GLS, kampuni iliyokuwa na mkataba mnono na Wizara ya Ulinzi ya Marekani.

“Hawanijibu, hawanipi majibu yoyote,” ananiambia. “Wanasema mkataba wako ulisitishwa na Jeshi la Marekani na huwezi kupata nyaraka zako. Ni vigumu.”

Kipindi cha The World cha PRI kiliwasiliana na kampuni ya GLS huko Virginia juma lililopita na kuacha jumbe kadhaa, lakini hakuna ujumbe uliojibiwa.

Ibrahim anasema aliishi Syria kwa miaka michache, kisha akahamia mkoa wa Kurdi kaskazini mwa Iraq mahali alipofanya kazi kwa maficho. Lakini anasema kuwa mwarabu mgeni kule lilikuwa tatizo; Mamlaka za ki-Kurdi zilimwambia arudi Baghdad, lakini aliogopa kwenda.

Badala yake, alivuka mpaka kwenda Uturuki, alipokutana na mwanamke wa ki-Afghan mwaka 2014. Walifunga ndoa ya kidini. Ibrahim anasema mke wake aliweza kwenda Canada, lakini hawezi kwenda naye kwa sababu hawana cheti cha ndoa.

“Niko peke yangu. Mke wangu yuko Canada na dada yangu yuko Marekani,” Ibrahim anasema. Wazazi wake wake Uturuki na anasema dada yake anaweza kumpeleka Marekani ndani ya miezi michache, lakini inaweza kuchukua miaka kwake kupata ruhusa.

Kwa hiyo Ulaya ndio mahali anapodhani panamfaa sasa. Lakini kufuatia Makubaliano mapya ya Umoja wa Ulaya na Uturuki [5], haielekei kwamba ataruhusiwa kubaki. Umoja wa Ulaya una mipango ya kuwarudisha wakimbizi wote kama Ibrahim walioingia nchini humo kutokea Uturuki waende Ugiriki. Uturuki imekubali kuwachukua na kubadilishana nao kwa msaada na bakhshishi nyingine zinazifikia dola za Marekani bilioni 6.

Umoja wa Ulaya unasema makubaliano hayo yanaweza kuwakatisha tamaa watu kuwapa hongo watu wanafanya biashara ya kuwasaidia wahamiaji na hivyo kupunguza vitendo hivyo vinavyohatarisha maisha yao kwa kujaribu kuvuka mpaka isivyo halali kwenda Ugiriki kutokea Uturuki. Lakini wakosoaji wa mpango huo wanasema njia moja inapofungwa, nyingine inafunguliwa.

Most of the asylum seekers who have gotten stopped in Greece are Syrians escaping the war at home. Credit: Filip Warwick. Used with PRI's permission

Wakimbilizi wengi walioshikiliwa Ugiriki ni wa-Syria wanaotoroka vita nchini kwao. Picha: Filip Warwick. Imetumiwa kwa idhini ya PRI

Na maafisa wa haki za binadamu wanasema matokeo ya kurudisha watu wengi kwa pamoja ni kinyume cha ubinadamu na inaweza kusababisha uvunjaji wa sheria za kimataifa.

“Kila mtu anayetafuta hifadhi ana haki ya kufanyiwa uchunguzi hatua kwa hatua kwa kuzungatia maslahi ya mtu huyo,” Kamishna wa Baraza la Ulaya la Haki za Binadamu Nils Muiznieks alikiambia kipindi cha The World.

Anasema makubaliano ya Umoja wa Ulaya na Uturuki yanatishia kukiukika kanuni hiyo.