- Global Voices in Swahili - https://sw.globalvoices.org -

Global Voices Yashikamana na Watetezi wa Uhuru wa Kujieleza nchini Morocco

Mada za Habari: Moroko, Uandishi wa Habari za Kiraia, GV Utetezi

Jumuia ya Global Voices yataka haki kutendeka kwa watetezi saba wa uhuru wa kujieleza walioshitakiwa kutokana na wajibu wao wa utetezi.

Watetezi hawa saba wamekuwa wakitetea haki za binadamu, kuweka bayana maovu ya maafisa wa serikali pamoja na kudai utawala wa sheria nchini mwao. Watano kati yao wameshitakiwa kwa kosa la “kuhatarisha usalama wa ndani wa Taifa” na wawili wengine wameshitakiwa kwa kosa la “kupokea ufadhili wa fedha bila ya kushirikisha sekretarieti ya serikali”. Tunaitaka serikali ya Morocco kusimamia makubaliano ya haki za binadamu za kimataifa na hivyo kufuta mashitaka iliyofungua dhidi ya watu hawa saba.

Hisham Almiraat at the Global Voices Summit in Nairobi, 2012.

Hisham Almiraat akiwa kwenye mkutano wa Global Voices jijini Nairobi mwaka 2012.

Miongoni mwa walioshitakiwa ni Hisham Almiraat, ambaye ni mtabibu na kwa muda mrefu amekuwa mmoja wa wachangiaji wa jumuia yetu. Hatuwezi kuwa kimya katika mazingira hatari anayokabiliana nayo ndugu yetu. Hisham amekuwa mstari wa mbele kabisa katika ulimwengu wa kublogu nchini Morocco kwa takribani miaka kumi. Alikuwa mwanzilishi wa miradi kadhaa ya Uanahabari wa kiraia ikiwemo Talk Morocco [1] na Mamfakinch [2], na pia alifanya kazi kama mkurugenzi wa kitengo cha utetezi cha Global Voices. Akimudu vizuri kati ya kazi zake za kitaaluma na kufanya kazi za kujitolea, Hisham ametumia miaka yake mingi kujibidisha kuboresha maisha na uhai wa jamii ya watu wa Morocco akiwa kama mtetezi wa jumuia za kiraia na pia kama mtabibu.

Kama ilivyo kwa vyombo vingine vya habari [3] na makundi ya haki za binadamu [4] ulimwenguni, tuna hofu kuwa mashitaka haya ni jaribio la serikali ya Morocco la kuwanyamazisha wote wanaojaribu kuhoji kuhusu sera na utendaji wa serikali.

Hatulitazami hili kama ni hatari tu kwa rafiki na mwenzetu, bali pia ni hatari kwa malengo yetu mapana. Kama jumuia ya wanablogu na wanaharakati kutoka nchi zaidi ya 160, kila uchao tunatetea na kusihi haki ya msingi ya binadamu ya uhuru wa kujieleza, kwani tumekuwa tukiandika na kusambaza habari kutoka kwenye jamii ya watu wasioweza kusikika na wala kusikilizwa kwa urahisi kutoka ulimwenguni kote.

Tunawaomba washirika wetu wote kuunga mkono ujumbe wetu, pamoja na serikali kutoka nchi mbalimbali kuishinikiza serikali ya Morocco kuwajibika kwa matendo na mwenendo wake. #Justice4Morocco [5]

 

UUNGE MKONO WITO WETU

Thibitisha tamko la wazi [6] kutoka kwenye jumuia yetu [BOFYA HAPA ILI KUTHIBITISHA] [6]

Unga mkono kampeni hii kupitia mitandao ya kijamii kwa kutumia kiungo habari #Justice4Morocco [5]

Soma na sambaza habari kuhusu kesi hii:

soma na sambaza makala za Global Voices [10]

  zilizoandikwa na Hisham.