- Global Voices in Swahili - https://sw.globalvoices.org -

Bunge Lililoteuliwa na Jeshi la Thailand Lapiga Kura ya Kutokuwa na Imani na Waziri Mkuu

Mada za Habari: Asia Mashariki, Thailand, Habari za Hivi Punde, Siasa, Uandishi wa Habari za Kiraia
Image from the Facebook page of Yingluck Shinawatra. [1]

Picha kutoka kwenye ukurasa wa Facebook wa Yingluck Shinawatra.

Siasa za Thailand zimechukua sura mpya leo baada ya waziri mkuu wa zamani wa nchi hiyo kupigiwa kura ya kutokuwa na imani nae na bunge la nchi hiyo, lililoteuliwa na serikali inayoongozwa na kijeshi.

Bunge la nchi hiyo lilisimamia mchakato wa kupiga kura ya siri kumwondoa waziri mkuu huyo wa zamani Yingluck Shinawatra kwa tuhuma zinazohusina na mpango wa kununua mchele [2] uliokusudiwa kuwasaidia wakulima wadogo, mpango ambao aliusimamia yeye.

Katika mpango huo [3] serikali ilinunua mchele kwa wakulima wadogo kwa bei ya juu na kuuza katika soko la dunia. Lakini wakosoaji wake wanasema mpango huo ulikuwa na malengo ya kumpa umaarufu na ulitekelezwa ili kukisaidia chama cha Yingluck katika sehemu ya kaskazini mwa nchi hiyo.

Yingluck ni waziri mkuu wa kwanza mwanamke katika utawala wa kifalme wa nchi hiyo, kupitia muungano wa kisiasa unaoongozwa na chama cha Pheu Thai ulioshinda katika uchaguzi wa 2011. Hata hivyo, jeshi la nchi hiyo limetawala [4] Thailand tangu Mei 2014. Jeshi limeandika katiba mpya na kuteua vyombo kadhaa ili kutekeleza mabadiliko ya uchaguzi na kisiasa kama sehemu ya kurejea kwenye utawala wa kiraia. Bunge ni moja ya taasisi zilizoundwa na jeshi kwa malengo ya kuratibu kipindi cha mpito.

Kura hiyo ya kutokuwa na imani na waziri mkuu ni picha ya sauti ya jeshi kutaka kumzuia Yingluck kurejea kwenye siasa za nchi hiyo.

Hesabu kamili ya kura za siri zilizopigwa kwenye kura ya kutokuwa na imani na waziri mkuu: 190 kwa 18

Vikosi vya kijeshi vilikuwa kwenye hali ya tahadhari kuzunguka viunga vya bunge hilo wakati wa kikao hicho

Saa 2 asubuhi mbele ya bunge kulikuwa na idadi kubwa ya wanajeshi na polisi kuwadhibiti wapinzani. Maandamano yalipigwa marufuku

Yingluck amepinga uamuzi wa bunge, unaomzuia kuchaguliwa kushika madaraka yoyote ya umma kwa miaka mitano. Kadhalika, anakabiliwa na mashitaka [12] kadhaa ya jina (yanayohusiana na kashfa za ufisadi) yanayoweza kumfanya afungwe jela kwa miaka isiyozidi miaka kumi.

Yingluck ametoa tamko rasmi kwenye mtandao wake wa Facebook, baada ya kufuta mpango wake wa kuongea na waandishi wa habari jijini Bangkok kama ilivyoagizwa na vyombo vya dola.

MHUTASARI: Baada ya kuzuiwa kuongea na vyombo vya habari na Jeshi, Yingluck ametoa tamko rasmi kwenye mtandao wa facebook

Polisi katika Hoteli ya SC Park. Wanasema walifika kumwomba kiungwana Yingluck asifanye mkutano na waandishi wa habari

Nakala ya tafsiri ya tamko lake, kama ilivyoripotiwa na tovuti ya chama cha Pheu Thai [18], inasema: 

Ningepedna kusisitiza kwamba sina hatia. Ningependa kuwashukuru walio wachache bungeni kwa kupiga kura ya kupinga hatua ya kuniondoa madarakani. Ninawapongeza kwa ushujaa wenu katika kuendeleza kanuni haki. Pamoja na ukweli kwamba mchakato wa kupiga kura ya kutokuwa na imani na mimi ulikimbizwa na haki haikufuatwa kiasi kwamba haki zangu za msingi zilipuuzwa, haki ambazo raia wote wa Thailand wanastahili, ninaamini kwamba nilifanya kila nililoweza kujitetea.

Ninasisitiza kwamba Mpango wa Uuzaji wa Mchele una manufaa kwa wakulima na nchi kwa ujumla, na mpango huo haukuleta hasara kama inavyodaiwa. Takwimu zozote kuyapa uzito madai ya mpango huo kulisababishia hasara taifa zimepikwa ili kufanya nionekane nina hatia na zina ajenda ya siri ya kuondoa upinzani wa kisiasa. Mbaya zaidi, maisha ya wakulima wa mchele yamefanywa kuwa karata ya kisiasa.

Kuhusu mashitaka yaliyofunguliwa na Mwanasheria wa Serikali, waziri huyo mkuu wa zamani alisema,

Inasikitisha kwamba vingi nilivyovizungumza jana vimetokea leo tena. Saa moja kabla ya Bunge kupiga kura ya kuniondoa, ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali iliamua kufungua mashitaka ya jinai dhidi yangu kwa kuzembea kazini. Mashitaka hayo yanapingana na matamshi ya kiongozi wa mashitaka kwamba hakuna ushahidi wa kutosha. Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ni taasisi ambayo kwa muda mrefu imekuwa ikitimiza wajibu wake kuhakikisha kwamba haki inatendeka. Lakini bado, vitendo vyao katika suala hili vinaibua maswali mengi kuliko majibu.

Katika tamko lake, alilia na kile alichokiita kukosekana kwa demokrasia na utawala wa sheria, hususani kwa wakulima.

Wakati kura ya kumng'oa waziri mkuu haukuja bila kutarajiwa, baadhi walifanya uchambuzi wa hali hiyo.

Kadri mgongano mkubwa wa maslahi unavyozidi kuwa wazi, ndivyo watu zaidi wanavyozidi kuamka

Kung'olewa kwa Yingluck ni maigizo zaidi ya kuwa mchakato wa haki na unaokubalika

Ungejisikiaje kama unaamka siku moja, unajikuta ulikuwa unaishi kwenye nchi ya ‘mazombi’ inayoendeshwa na jeshi bila kuongozwa na sheria wala haki na uhuru wa kiraia

Thailand ni Bangkok na Bangkok ni Thailand. Kura ya kutokuwa na imani kwa gharama za nani?

Nyakati ngumu zinanukia, na kadri nchi inavyozidi kuwa chini ya jeshi, bila kuwa na ushiriki wa raia kwenye utawala na uwajibikaji, upinzani hautakoma.