- Global Voices in Swahili - https://sw.globalvoices.org -

Shindano la Insha GV: Namna Gani Sera za Intaneti Zinaathiri Jamii Yako?

Mada za Habari: Uandishi wa Habari za Kiraia, GV Utetezi
Group photo from Global Voices 2012 Summit in Nairobi, Kenya.

Picha ya wahudhuriaji wa Mkutano wa Global Voices uliofanyika Nairobi, Kenya mwaka 2012.

Namna gani maamuzi ya kisera ya mashirika makubwa na serikali yanawaathiri watumiaji wa intaneti? Mradi wa Advox wa Global Voices ungependa kusikia mitazamo ya mtandao wetu wa wanablogu, wanaharakati na wataalumu wa uandishi wa kiraia kuhusu suala hili, kwa mtindo wa  insha .

Kama sehemu ya mkutano wetu wa GV mwaka 2015, tunaikaribisha jumuiya na washirika wetu kuandika na kutuma  insha zinazoeleza  — kwa lugha nyepesi — madhara halisi ya sera zinazohusiana na matumizi ya intaneti kwa wananchi katika nchi au maeneo fulani. Sera zaweza kuwa zile zinazotungwa na serikali, vyombo vya kimataifa au hata makampuni ya kiteknolojia. Kinachotakiwa ni kueleza namna sera hizo zinavyowaathiri raia (wanaharakati, wanablogu, waandishi wa habari au watu wengine) katika kutumia mtandao wa Intaneti kwa malengo ya kuongeza upatikanaji wa habari, kuibana serikali iwajibike au hata kulinda haki za binadamu.

Hoja zinaweza kujengwa kwenye maeneo mengi kama vile mipango ya serikali kuwadhibiti watu, ufuatiliaji/udukuzi wa mitandao ya kijamii, Haki ya kusahauliwa na hata hali ya kutokuwa na upendeleo. Sababu kuu ni kwamba serikali, makampuni, na wadhibiti wana madhara makubwa sana kwa kile tunachoweza kufanya au kutokukifanya mtandaoni. Kama jumuiya, tunalitambua suala hili vizuri sana – na tunajua kwamba ili kuyaelewa matukio ya kudhalilishwa, kukamatwa au hata kutambua chimbuko la sera hizi na namna zinavyoumbika, ni muhimu kutambua siasa za nchi husika, uchumi wake na hata historia yake. Tuna fursa ya kueleza masimulizi haya.

Hatutafuti sana uchambuzi wa kitaalamu au tafiti za kina na badala yake tunaangalia maelezo yanayoshawishi kuhusu changamoto za haki ya uhuru wa kujieleza na faragha ya mtandaoni, katika namna ambayo kila mtumiaji wa mtandao wa intaneti anaweza kuyaelewa.

Lengo la  shindano hili ni kukuza sauti na mitazamo ya jamii yetu, kusaidia dunia ione madhara ya sera. Tunakusudia kutunuku maandishi na fikra zitakazojitokeza kuwa bora kwa kuzitambua kwa heshima yake katika mkutano wa Global Voices 2015. Washindi watazawadiwa Dola za Kimarekani $1000 (zawadi ya kwanza), $500 (zawadi ya pili) na $250 (zawadi ya tatu). 

Tunayo bahati ya kuwa na kikundi cha watetezi wa mtandao huru na wataalamu wa sera kutoka duniani kote watakaoungana nasi kuwa majaji wa shindano hili.  Shindano hili linafadhiliwa kwa fedha zilizotolewa na Google, mmoja wa wadhamini wa Mkutano wa Global Voices 2015.

Tafadhali tuma insha yako yenye maneno kati ya 800 na 1400 kwa kutumia fomu hii [1]. Insha zinaweza kutumwa kwa lugha yoyote kwenye tovuti hai za [2] Global Voices. Tutazichapisha  insha hizo kwenye tovuti ya Mkutano wa Global Voices 2015, chini ya leseni ya Haki miliki 3.0 ya Creative Commons. Tutazipokea insha zilizotumwa kati ya August 1, 2014 mpaka  Desemba 7, 2014. Mwisho wa kupokelewa insha hizo ni saa 11:59 PM kwa Majira ya Pasifiki (UTC-7) siku ya Desemba 7, 2014.

Tuma insha yako hapa! [1]