
Mheshimiwa Joseph (Sugu) Mbilinyi akipinga jaribio la kutaka kutolewa ndani ya ukumbi wa Bunge na maafisa usalama wa Bunge wiki iliyopita. Picha kwa idhini ya jamii forums.
Kwa miaka ya hivi karibuni, bunge la Tanzania limekuwa na mfululizo wa matukio ya kustaajabisha na vituko mithili ya maigizo. Kulipuka kwa majibizano yasiyo ya mpangilio yanayofuatiwa na wabunge kutoka nje ya bunge, ambao mara nyingi huwa ni wabunge wa vyama vya upinzani, imesababisha vikao vya bunge kuwa ni miongoni mwa vipindi vya televisheni visivyochosha kuangaliwa.
Kwa mfano, Aprili 2011, Ezekiel Wenje, mbunge wa kwa tiketi ya chama kikuu cha upinzani, CHADEMA aliamsha hasira ya spika Anna Makinda kufuatia matamshi yake kuwa baadhi ya nyadhifa fulani za serikali zinachaguliwa kupitia “njia za udanganyifu”. Wabunge wa chama tawala, Chama cha Mapinduzi (CCM) walipinga na kumtaka Wenje kufuta kauli yake. Alikataa kufanya hivyo, hali iliyosababisha azomewe na wabunge wa Chama cha Mapinduzi.
Kama mwanablogu wa Kitanzania, Subi alivyoandika yaliyosikika wakati wa majibizano, inasemekana Wenje alisema “tufunge mlango tupigane”.
Hali haikufika huko, kwani Wenje alifuta kauli yake na taratibu za bunge ziliendelea kama kawaida. Lakini kuliendelea kuwa na maneno ya ugomvi wa hapa na pale. Februari 2013, kikao cha bunge kilichokuwa kikirushwa moja kwa moja tokea bungeni ilibidi kisitishwe kuoneshwa kufuatia vurugu zilizoibuka Bungeni humo . Ndipo, miezi mitano tena baadae, lilipotokea tukio la mbunge wa Chadema kutolewa nje ya ukumbi wa Bunge kwa kuingilia hotuba ya mbunge mwenzake kutoka chama tawala, CCM wakati wa mjadala wa bajeti ya serikali.
Wiki hiyo hiyo, Bunge, kama lilivyozoeleka kuitwa, lilishuhudia tukio la aibu na la kushitua ambalo halitakaa lisahaulaike. Mheshimiwa Peter Serukamba, mbunge kwa tiketi ya CCM, aliwatukana wabunge wenzake mara baada ya kuonesha kumdhalilisha pale alipokuwa akisimama ili azungumze. Kupitia tovuti ya Bongo5.com,
Tusi la Serukamba, “f**k you'”, lilipelekea mmoja wa wapiga kura kutoka katika jimbo la Serukamba, aliyejitambulisha kwa jina la Dr Mvano Khalidi, kutoa maoni yake kwa kuomba msamaha kupitia ukurasa wa Facebook kufuatia utovu wa nidhamu wa mbunge wake:
Poleni sana waheshimiwa wabunge kwa kutukanwa ila tunaomba rathi kwa niaba ya wana Kigoma wote kwa kosa alilolifanya mbunge wetu kutoka kigoma ulimi ulitereza jumani hayakuwa makusudio yake kusema vile mimi kuma mzalendo wa mkoa wangu.
Siku ya Alhamisi, Septemba 5, 2013, mambo yaliendelea kuwa mabaya zaidi. Mbunge wa chama cha upinzani cha Chadema, Mheshimiwa Joseph Mbilinyi, alijikuta katika wakati mgumu pale alipokuwa akikabiliana kwa nguvu na majibizano na maafisa usalama wa bunge, tukio lililokuwa la kushangaza na la kuwaacha watu midomo wazi.
Tukio hili lilianzia pale Mbilinyi, ambaye ni msanii mkongwe wa miondoko ya hip hop aliyehamia kwenye siasa , pamoja na wenzake wa chama chake walipokataa kutii amri ya kutoka nje ya ukumbi wa bunge iliyotolewa na Naibu wa Spika, Job Ndugai.
Hali ilifikia hapo mara baada ya kiongozi wa kambi rasmi ya upinzani Freeman Mbowe, kukataa kukaa hata baada ya kutakiwa kufanya hivyo na Ndugai. Kutoka katika gazeti la The Citizen:
Bwana Ndugai alitoa amri kuwa, kiongozi wa kambi rasmi ya Upinzani atolewe katika ukumbi wa Bunge kwa kukataa kutii amri ya kukaa. Bwana Mbowe alipinga harakati za Naibu Spika za kutaka kumzuia Mbowe asiendelee na msimamo wake wa kutaka kuhamisha mjadala ili kusitisha mjadala wa Rasimu ya mapitio ya mabadiliko ya Katiba ya mwaka 2013.
Punde, machafuko yalianza mara baada ya wabunge wengine wa upinzani kwenda kumkinga kwa kumzunguka bwana Mbowe ili kuzuia maafisa wa usalama wa bunge wasimtoe Mbowe Bungeni.
Katika jukwaa maarufuJamii Forums, picha zilimuonesha Mbilinyi akikataa kuondolewa katika ukumbi wa bunge na maafisa usalama, uliibua mjadala wa kina kuhusiana na aina ya siasa ya Tanzania. Mchangiaji mmoja aliyejitambulisha kwa jina la “Stoudemire” aliuliza swali hili:
Namna hii kweli tuwape vijana nchi kweli? [Mbilinyi ni mmoja wa wabunge wadogo kabisa] Waacheni wazee wasinzie bungeni tu inatosha!
Mchangiaji mwingine mwenye jina Tata alipendekeza kuwa, tukio zima limesababishwa na Naibu spika kushindwa kuongoza vyema kikao cha bunge. Tata pia alitanabaisha kuwa, hali iliyooneshwa na Mbunge Mbilinyi naweza kuwa ilisababishwa na hamasa kutoka kwa wenzake:
Amenifurahisha huyu Naibu Spika kwa kudai ni aibu ya kiongozi wa Upinzani kuongoza wapinzani kutoka nje wakati kimsingi hii ni aibu yake kwa kushindwa ku-manage [kuongoza vyema] kikao…la hii move [tukio] ya mwisho ya huyu mheshimiwa Sugu imeniacha hoi kwa kicheko. Inaonekana jamaa ama alikuwa amepata “chang'aa” au alikuwa amevuta haya masigara yanayopendwa na vijana.
Katika mtandao wa Twita, Sajjad Fazel (@SajjadF) alihoja kuwa, tukio hilo linaweza kuwa limeshusha hadhi ya chadema:
@jjmnyika Sasa alichofanya Mh. Joseph Mbilinyi, Inaonyesha picha mbaya saana kwa CHADEMA na kwa wa Tanzania wote.
Katika Ulimwengu wa Blogu, kipande cha video kutoka katika kituo cha Televisheni cha ITV kilisambaa, kiasi cha kufanya tukio hilo kuweka kumbukumbu ya kudumu na kutokusahaulika daima. Kupitia GongaMx:Kwenye makala yake ya mwaka 2011, Subi alitoa tahadhari:
Huenda…Bunge la Tanzania lingeingia kwenye orodha ya viroja vya Wabunge wa Mabunge (kama haya, bofya hapa utizame video kwenye mtandao wa Youtube) kuonyesha namna wabunge wa nchi mbalimbali Duniani walivyowahi kupandwa jazba kiasi cha kujikuta (pasina kufahamu) wanageuza kumbi za Bunge kuwa viwanja vya ‘masumbwi’
Kwa tukio la hivi karibuni, Subi amethibitisha kuwa sahihi kufuatia tahadhari aliyoitoa takribani miaka miwili iliyopita.
UPDATE: Katika historia ya yanayojiri katika Bunge la Tanzania, tukio lililotokea mwaka 2008 ni vyema sana likajumuishwa. Ifuatayo ni ripoti ya mwanahabari wa Blogu ya Mikocheni Report, Elsie Eyakuze akitoa maelezo ya tukio hilo :Jaji Mkuu mstaafu, waziri wa zamani wa Wizara ya Miundo Mbinu, hivi sasa akifahamika kama mmiliki wa vibilioni vichache [vijisenti], Bw Andrew Chenge alinaswa na kamera za bunge( CCTV) siku chache zilizopita muda wa usiku katika ukumbi wa bunge akifanya jambo lililotiliwa mashaka makubwa. Mheshimiwa [the right honorable] alinaswa na kamera hizo zilizomuonesha akiingia bungeni masaa kadhaa baada ya kusindikizwa na mfanyakazi wa bunge na kisha kuonekana akinyunyiza kitu kwenye viti vyote vya wabunge. Alitumia muda mwingi zaidi akizunguka-zunguka katika kiti cha Spika. Ninahisi hayakuwa marashi.
Kwa wakati huo, Chenge alikuwa akichunguzwa na taasisi ya kuchunguza makosa makubwa ya jinai nchini Uingereza (SFO) kufuatia kutuhumiwa kwa kosa la rushwa iliyohusisha kampuni ya kiingereza ya BAE.
Miaka minne baadae, mara baada ya Tume ya Kupambana na Rushwa ya Tanzania ‘kushindwa’ kuweka bayana makosa aliyotuhumiwa nayo Mh. Chenge, Mkurugenzi wa mashitaka alifutilia mbali mashitaka hayo.
Hata hivyo, haikuweza kufahamika moja kwa moja, alichokuwa anakikifanya Chenge katika ukumbi wa Bunge. Lakini, kwa mujibu wa Eyakuze, ilionekana kuwa, jaji huyo Mkuu mstaafu aliamua kutumia njia za giza katika harakati za kutaka kujinasua kwenye mashitaka yaliyokuwa yakimkabili:
Bw. Chenge, mbuzi wako anachomwa. Vifaranga wako wameshafika nyumbani na sasa wanajikusanya kwenye kiota. Unakivuna kile ulichokipanda n.k Ulichokiacha katika macho ya watu hadi wakati huu ni kiasi kidogo sana cha sehemu ya utu wako, kitu ambacho sote kwa hiari tulikubaliana na wazee wenye pesa na vitambi. Nashauri uendelee kung’ang’ania tena kwa mikono yote miwili. Kusaliti wenzako na kutaka kuwabiga juju wabunge wenzako sio utaratibu mzuri wa kutatua yanayokusibu.
Chenge bado yupo bungeni na kwa sasa ni Mwenyekiti wa kamati ya Bajeti ya Bunge.