- Global Voices in Swahili - https://sw.globalvoices.org -

Bi Harusi wa Miaka 14 Huko Malaysia

Mada za Habari: Asia Mashariki, Malaysia, Haki za Binadamu, Uandishi wa Habari za Kiraia, Vijana

Hivi karibuni ilitolewa taarifa [1] kwamba ndoa ya kupangwa kati ya msichana mwenye umri wa miaka 14 na mwalimu mwenye umri wa miaka 23 ‘ilianzisha wito wa mjadala mpya juu ya ndoa za watoto wadogo’. Chini ya sheria ya Syariah ya Malaysia, ambayo i8na mamlaka juu ya Waislamu, Waislamu walio chini ya umri wa miaka 16 wanatakiwa kupata idhini ya mahakama ya Syariah kabla ya ndoa kuruhusiwa. Katika shauri hili, mahakama ilitoa ruksa kwa watu hao wawili kufunga ndoa.

Glenda Larke anaamini [2] kwamba ndoa za watoto hazina tofauti na ngono batili kati ya watu wazima na watoto, hata kama ni kwa mujibu wa sheria.

Mtoto wa shule mwenye umri wa miaka 14 siyo mtu mzima. Si mwanamke kamili, hata kama ameshaanza kupata hedhi. Bado ni mtoto mdogo. Anafuata uongozi wa watu wazima. Dini yake na utamaduni wake unauelekeza kutii wakubwa wake, hasa wazazi wake. Hajaerevuka na hana kinga.

Mwanaume mwenye mika 23 mbaye anamuoa – mwanaume mwenye elimu, ambaye si mtu fulani asiyejua kusoma ambaye jamii yake bado imejikita katika fikra ya karne ya 19 kwamba watoto wanapaswa kuanza kufanya kazi wakiwa na umri wa miaka 12 na kuolewa wakiwa na miaka 14 – kwa ujumla na wazi, ni mfanya ngono na watoto wadogo.

B.Joe anaona [3] kwamba haki za watoto na vijana chini ya umri wa miaka 18 hazifuatwi na mahakama ya Syariah pamoja na wazazi wa msichana huyo.

Na sehemu inayochekesha katika makubaliano yote haya ni kwamba ndoa hiyo ilipitishwa na mahakama ya Syariah – je nini kimezitokea kinga za vijana chini ya umri wa ridhaa? Kwa nini wazazi hawakuweza kusubiri kwa miaka mingine michache mpaka hapo mtoto Yule atakapoweza kufanya uamuzi yeye mwenyewe?

Un:dhimmi pia anaamini [4] kuwa jambo hili ni kosa kimaadili.

Tafiti baada ya tafiti zinaonyesha kuwa wasichana wanaofanyishwa vitendo vya ngono katika umri wa mapema hivyo hupata madhara si tu katika mfumo wao wa uzazi ambao bado unakua, lakini pia hupata athari za kisaikolojia za muda mrefu.

Hata hivyo, Fyzal alichukua msimamo usiofungamana na upande wowote [5] katika suala hili.

Katika hali hapo juu ridhaa ya mahakama ya Syariah ilipatikana. Na ina maana kwamba tunapaswa kuwa na imani katika Mahakimu wa Syariah – ni lazima walizingatia mazingira yote kabla ya kutoa ridhaa.

Ridhaa kama hiyo, ninaamini, ilitolewa na mahakimu wakiwa na imani kwamba mwanaume Yule atamuangalia vyema msichana na msichana huyo atakua vizuri chini ya uangalizi wa mwanaume huyo. Ikiwa mahakimu wangetia shaka, ridhaa ya namna hiyo isingetolewa.

Kwa hiyo, nawasilisha kuwa katika masuala ya ndoa kati ya wasichana wa Kiislamu walio chini ya umri wa miaka 16, tuziachie mahakama za Syariah zifanye kazi yake. Wanafahamu ni wakati gani wa kutoa ruksa na wakati gani wa kutotoa ruksa.

Lakini nina mtazamo kuwa majadiliano ya wazi bado yanatakiwa kati ya serikali na wataalamu wa Syariah ili kutatua suala hili.