Lebanon: wanablogu washinikiza jarida la Daily Star kubadilika

Picha imepatikana kutoka http://betterdailystar.blogspot.com/

Picha imepatikana kutoka http://betterdailystar.blogspot.com/


Umewahi kutembelea Jarida la Kiingereza la mtandaoni la Lebanoni, The Daily Star?

Kwa mujibu wa mwanablogu maarufu, Qifa Nabki, jarida hili ni:

…moja ya wavuti mbaya zaidi nilizowahi kuziona. Iko taratibu sana, ina mambo mengi yasiyopangiliwa, na ina sura mbaya.

Mwanablogu mwingine, Richard Hall, anaielezea tovuti ya The Daily Star:

…ni rahisi sana kuipitia kama ile boti ya moshi ya Kirusi ya miaka ya 1920.

The Daily Star, Jarida pekee la Kiingereza la Lebanon, limekuwa likitoa habari za mtandaoni kutoka Beirut kwa zaidi ya mwongo mmoja. Tangu kuzinduliwa mtandaoni, gazeti limegoma kufanya wavuti hiyo iendane na wakati, ikiwachanganya wasomaji wake.

Jarida ‘baya’ la Daily Star limewafanya wanablogu wa Kilebanoni kuchukua hatua, kwa kampeni ya mtadaoni iliyozinduliwa na mbunifu wa blogu ya Beirut Spring, Mustapha.

Mustapha ametengeneza kwa werevu wavuti ya kuigiza ya Daily Star- Mradi wa daily Star ulio bora zaidi au #BDSP kwenye twita –akitumia nyenzo ya WordPress kuonyesha uwezo duni wa timu ya Teknolojia ya Habari (TH) na wabunifu wa wavuti wa The daily Star.

Ingawa alichokifanya kinaweza kuwafanya watu kufungua macho yao dhidi ya The daily Star, Mustapha anasisitiza kwamba nia yake ni chanya:

-Nia ya #BDSP si kuwaiba wasomaji wa wavuti ya The Daily Star. Ni kuwarudisha wasomaji walioacha kuisoma kwa kukata tamaa. Kwa hakika, jarida hili lingepaswa kutulipa kwa kufanya hivi:)

-Mradi huu haukukusudiwa kwa namna yoyote kuharibu sifa ya Daily Star. Hoja ya mradi huu ni kujaribu kuielekeza tovuti ya daily Star kutoka kwenye kile tunachoamini ni mrengo usiosahihi.

-Wakati daily Star watakapoweka tovuti bora zaidi badala ya hii iliyopo, mradi huu hautakuwa na haja tena ya kuwepo. Lengo letu litakuwa limetimia. Kwa hakika tutageuka kuwa mashabiki wakubwa wa mstari wa mbele.

-Tunaheshimu kabisa haki miliki za kitaaluma. Hatujajidai kumiliki kitu hiki au kudai eti tuliandika makala. Hii ndio maana mradi huu unajitahidi kuweka majina ya sahihi ya wachangiaji kwa kila makala.

Kwa nini nafanya hivi. Suala ni nini?

Naam, ninajaribu kusema hivi: kama jamaa mmoja (wako mnyenyekevu) anaweza kutumia kwa uhuru programu zinazopatikana wazi (wordpress kama utataka kujua) ili kutengeneza mbadala huu, tena tovuti bora zaidi kuliko yao ndani ya majuma mawili, kwa nini gazeti hilo na Idara yao ya Teknolojia ya Habari wasifanye hivyo? Kwa maneno mengine, ninamaliza majadiliano kwamba eti itakuwa ghali sana kufanya hivyo. Nisikilizeni: Wamekuwa wavivu tu.

Lakini je, hii si kinyume cha sheria?

Inawezekana. Lakini sitengenezi fedha yoyote kwa njia hii (kwa hakika, ninalipa kiasi fulani katika jitihada na ada ya kutunziwa wavuti hii), na naahidi kwamba mara tu watakapofanya kitu kwa tovuti yao, nitajiondoa kwa furaha. Hata hivyo, itawagharimu kunifungulia mashitaka mimi zaidi ya (gharama za) kurekebisha wavuti yao na kunifanya niondoke migongoni mwao.

Jitihada za Mustapha hakika zilikamata macho ya wanablogu wengi wa Kilebanoni wanaomuunga mkono.

Rami kwenye +961 aliongeza maneno machache kuunga mkono kwenye blogu yake:

Nini cha kufanya unapokuwa umechoshwa kusubiri kitu kutokea? Kitu bora ni kulichukua jambo mikononi mwako! Na hivyo ndivyo mwanablogu mwenzetu Mustapha amefanya wakati akisubiri watu wa Teknolojia ya Habari wa Daily Star kuirekebisha tovuti yao.

Kama alivyofanya Tajaddod Youth:

Wakati tumo kwenye somo la tovuti zisizofanya kazi, baada ya miaka mingi ya wazungumzaji wa Kiingereza kuchoshwa na tovuti ya Daily Star, mwanablogu mmoja ameamua kuchukua hatua.

Matokeo, si tu ukosoaji dhidi ya visingizo dhaifu kwa tovuti ya jarida pekee la Kilebanoni linaloandikwa kwa lugha ya Kiingereza, lakini ni ubunifu mpya kabisa wa ukurasa wa kufikia wa jarida hilo ambao wote tunaupenda.

Maoni ya kuunga mkono kwenye #BDSP yalimiminika kwenye posti ya blogu ya Qifa Nabki juu ya mada hiyo:

Black Star anasema:
Aisee. Ninajisikia naweza kuvuta pumzi!
Kwa nia njema kabisa NINAICHUKIA wavuti ya Daily Star kama ilivyo sasa (hivi inaonekana ajabu kuisoma kunanifanya nijisikie kubanwa?)

Sean Anasema:

Maboresho makubwa. Tovuti halisi inatisha sana. Inaonekana kama blogu ya kuongezwa moja kwa moja na wavuti zisizo na mmiliki zenye matangazo mengi, au hata mbaya zaidi.

Wasomaji wengi wa Daily Star watakuwa wakitegemea kwamba kampeni ya #BDSP itasababisha mabadiliko kwenye jarida husika, kuigeuza ile boti ya moshi ya Kirusi ya miaka ya 1920” kuwa boti ya kisasa ya karne ya 21.

Kadhalika katika Global Voices Online:

Lebanon: Mradi wa Jarida Bora la Daily Star

Anza mazungumzo

Mwandishi, tafadhali jiandikishe »

Miongozo

  • Tafadhali wape heshima watumiaji wengine. Maoni yenye lugha ya chuki, matusi na mashambulizi binafsi hayataruhusiwa.