- Global Voices in Swahili - https://sw.globalvoices.org -

Rais wa Malawi kutangaza rasmi penzi lake siku ya Valentine

Mada za Habari: Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara, Malawi, Sanaa na Utamaduni, Uandishi wa Habari za Kiraia, Utawala, Vichekesho

Wamalawi wanatafakari taarifa kuwa mnamo tarehe 1 Mei, rais wa nchi Dkt. Bingu wa Mutharika anatarajiwa kumuoa waziri wa zamani wa utalii Callister Moyo. Harusi hiyo itatanguliwa na sherehe za kitamaduni za uchumba wakati wa siku ya wapendanao ya Valentino tarehe 14 Februari. Wanabloga wachache wamemtakia heri rais katika mapenzi mapya aliyoyapata baada ya kifo cha mkewe Ethel [1] miaka mitatu iliyopita.

Emmanuel Sobilika
wa Malawi Digest [2] anaandika:

Katika taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa Jumatano ambayo Malawi Digest iliruhusiwa kuisoma, Ikulu inasema kuwa Rais Mutharika anatarajiwa kumuoa Chimbombo katika Mei mosi, 2010.

Hata hivyo, kabla ya kufunga ndoa rasmi, wawili hao watakuwa na sherehe zxa kitamaduni za uchumba tarehe 14, Februari 2010. Tarehe 14 Februari ni siku kimataifa ya Valentino ambapo watu husherehekea mapenzi na wale wanaowapenda.

Taarifa hiyo rasmi inaweka wazi kuwa wote, Dkt Mutharika na Bi Callista Chapola Chimombo ni wajane. Ikulu inaeleza kuwa wote Dkt Bingu wa Mutharika na Chimombo ni waumini wa kanisa Katoliki la Roma.

Mwanahabari Kondwani Munthali anampongeza [3] rais kwa kile alichokiita:

Kuongoza njia kwa kutangaza nia ya Ndoa Takatifu, na kuongeza tunatumaini kuwa nitapata kadi na kuwaonyesha marafiki zangu wengi picha za tukio hilo

Callista alionekana katika dhifa nyingi za kitaifa akiwa ameketi pembeni ya rais. Awali alikanusha habari za mapenzi. Maofisa wa Ikulu pia walikataa kufanunua itifaki na uhalali wa waziri huyo wa zamani kuwa Karibu sana na rais katika dhifa za kitaifa. Richard Chirombo [2] aliye katika jiji la kibiashara la Malawi, Blantyre aliandika:

Kuanzia katikati ya mwezi Disemba 2009 Chimombo amekuwa akiketi pembeni ya Mutharika, nafasi inayotengwa kwa maofisa wa juu serikalini na maswahiba wanaoaminiwa. Badala yake, Chimombo anasema kuwa ni rais ambaye huamua ni nani anayeketi pembeni yake, na kwa hiyo ilikuwa ni “ustahiki” kwamba Mutharika alimruhusu kuketi Karibu naye.

Hii itakuwa ni harusi ya pili ya taifa [4] nchini Malawi baada ya ile ya Bakili Muluzi mwaka 1999.