- Global Voices in Swahili - https://sw.globalvoices.org -

Austria: Jinsi Nyenzo Za Habari Za Kijamii “Zinavyoviwashia Moto Vyuo Vikuu”

Mada za Habari: Ulaya Magharibi, Austria, Ujerumani, Elimu, Harakati za Mtandaoni, Maandamano, Uandishi wa Habari za Kiraia, Vijana

Je, ulijua kwamba katika wakati huu vyuo vikuu vingi kote Ulaya vinakaliwa na wanafunzi? Maelfu ya wanafunzi hao wanalala, wanapika, wanafanya mijadala na sherehe kwenye kumbi za mikusanyiko kuandamana wakipinga kutolewa kwa ruzuku ndogo kwa mfumo wa elimu na kile kinachoitwa mchakato wa Bologna [1], sera ya elimu ya Umoja wa Ulaya.

Kilicho cha tofauti kuhusu maandamano haya ni ukweli kwamba hayakuratibiwa na vyama vya wanafunzi lakini yameandaliwa kwa kuanzia chini kwenda juu, kwa msaada wa vyombo vya habari vya kijamii mtandaoni.

Yote hii ilianzia Vienna, Austria, tarehe 22 Oktoba, ambapo kikundi kidogo cha wanafunzi walikutana ili kufanya maonyesho ya kushtua [2] katikati ya jiji kwa ajili ya kupinga, na baada ya hapo wakaelekea kwenye Chuo Kikuu cha Vienna ambapo walijaza kwa haraka na bila kupanga Ukumbi wa kukutania. Wakati polisi wanawasili, habari za tukio hilo zilikuwa zimesambaa tayari kwenye Twita, zikihamasisha waungaji mkono wengi zaidi kiasi kwamba haikuwezekana kuwaondoa katika ukumbi.

Tovuti ya Unsereuni

Tovuti ya Unsereuni


Ndani ya siku chache, waandamanaji hao waliofanya makazi –kwa msahangao wao –waliusimika muundo wa uongozi makini: Uhamasishaji na mawasiliano yalifanyika kwa njia ya alama hii ya Twita [3]: #unibrennt [4] na #unsereuni [5] (“Chuo Cikuu kwawaka moto” na “Chuo chetu Kikuu”)

Matangazo ya mtandaoni [6] kwa masaa 24 kutokea kwenye ukumbi huo yalizinduliwa. Majukumu ya kiutawala kuanzia kupika mpaka kufanya usafi yalitengenezwa kwa kupitia wiki [7] na yaliwasilishwa kwa umma kwa njia ya wavuti [8]. Twita, Blogu na Facebook [9] (mashabiki 32, 400 mpaka sasa) walitumika kusambaza ujumbe.

Hili lilikuwa na matokeo mawili:

-Kwa mara ya kwanza waandamanaji wa kiwango hiki hawakuhitaji kuungwa mkono na vyombo vya habari vya kale kwa ajili ya uhamasishaji. Ndani ya juma moja baada ya kuanza kwa maandamano, zaidi ya waandamanaji 20,000 walivamia mitaa ya Vienna, wakitangulia kabla ya habari za vyombo vya habari vya kale. Mawasiliano ya Vyombo vya habari yalikuwa kwa kiasi cha kuwa kidogo sana (jambo ambalo lilisababisha mkanganyiko mkubwa). Wanafunzi hawakuhitaji chombo chochote cha habari cha kale na kwa sababu waandamanaji hawakuwa na ngazi za kiuongozi, na pia palikuwa na upungufu wa wasemaji wakuu.

-Pili, kwa sababu kila mmoja aliweza kufuatilia kilichokuwa kinaendelea ndani ya Ukumbi wa kukutania (matangazo ya mtandaoni yalipata watazamaji nusu milioni ndani ya mwezi mmoja) ilisababisha vyombo vya habari kushindwa kuwapachika jina waandamanaji kama wafanya ghasia au watu wenye msimamo mkali. Watu wengi walijua haikuwa kweli. Nguvu ya kutoa maoni imegeuka.

Mara maandamano yaliambukizwa kwenye Vyuo Vikuu vya miji mingine nchini Austria na nje ya nchi: Leo, kwa chini ya mwezi mmoja na nusu baada ya maandamano ya kwanza, kadri ya vyuo vikuu 100 nchini Austria [10], Ujerumani, Uswisi, Albania, Serbia, Ufaransa, Italia, Kroashia, na Uholanzi vimekaliwa ama vimeshuhudia namna nyingine ya uandamanaji mkubwa.

Katika blogu ya Wissen belastet [11], Max Kossatz, mwanablogu na mwangalizi wa vyombo vya habari kutoka Austria, amechambua [12] mkondo wa Twita: Wenye maingizo 66,379 yaliyofanywa na watumiaji zaidi ya 6,780 yamechapishwa juu ya mada hiyo kwa mwezi uliopita. Picha 1,043 zilitundikwa kwenye sehemu ya picha ya Twita na kuvutia watazamaji 125,612 – tazama haya kwenye Twitpic photo mashup kwenye Youtube [13]. Na kinachofurahisha zaidi, ni ramani za kufuatilia maingizo kuonyesha namna maandamano yanavyosambaa kadri muda unavyoenda (tazama kwenye HD kwa ukubwa wa skrini yako ili upate uhondo kamili):

Gerald Bäck wa Bäck Blog [14], anayefanya kazi ya biashara ya uangalizi wa vyombo vya habari, aligundua kuwa idadi kuu ya maingizo ya Twita, yaani idadi maalumu ya wafuatiliaji yanayoipata wao, ilikuwa 386,860. Uchambuzi wake [15] [de] unaonyesha akina nani walikuwa wahamasishaji wakuu, anuani za URL zilizounganishwa zaidi kwenye alama zipi (hashtags) za Twita zilitumika zaidi.

Katika Blogu yake, smime [16], Michael Schuster ambaye ni mtaalamu wa teknolojia ya kublogu na mchambuzi wa muundo wa lugha, alichangia kwenye mapitio [17] [de] ya namna “vyombo vya habari vya kale” vilivyoripoti matukio hayo. Alihesabu, makala 2,700 na kutambua miendelezo minne iliyokuwa ikiachiana zamu kwa takribani juma moja kila mmoja: “Maandamano yafanyika”, “Maandamano yaendelea”, “Maandamano yasambaa”, na hivi majuzi, “Sawa, imetosha sasa.”

Luca Hammer wa blogu ya 2-Blog [18], mwanafunzi na mtaalamu wa nyuma ya pazia wa harakati za mtandaoni mjini Vienna, amechapisha taarifa [19] [de] ya namna matangazo ya wiki, Twita na matangazo ya mtandaoni yalitumika kufanya mambo yaende.

Inaonekana kama suala la #unibrennt [4] linaweza kuwa hatua ya awali ya mabadiliko ya siasa za Austria kwa matumizi ya nyenzo za kijamii za mtandaoni. Suala hili limejenga uelewa mpana –na hata kuchanganyikiwa –baina ya miundo iliyopo ya vyombo vya habari na siasa, na kujenga ari ya kuwezeshwa miongoni mwa wanafunzi na viongozi wa kidijitali.