- Global Voices in Swahili - https://sw.globalvoices.org -

Uganda: Mradi wa Katine Wawafikisha Wanakijiji Kwenye Ulimwengu wa Blogu

Mada za Habari: Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara, Uganda, Elimu, Maendeleo, Vyombo na Uandishi wa Habari

Inakadiriwa kuwa matumizi na kuenea kwa intaneti nchini Uganda ni kwa kiwango cha asilimia sita tu, idadi ambayo inazuia sehemu kubwa ya watu kujiunga na ulimwengu wa blogu nchini Uganda au kuweza kuwasiliana na ulimwengu wa blogu duniani. Mradi wa Katine [1]unaoendeshwa na Guardian and Observer unafanya kazi kubadilisha hali hiyo katika kijiji kimoja.

Tangu mwezi wa Kumi 2007, mradi wa Katine umefuatilia matokeo ya mradi wa maendeleo wa AMREF [2] wa kiwango cha pauni milioni 2.5 (dola milioni 4), katika Katine [3], kitongoji kimoja cha kaskazini mashariki ya Uganda (talii kwenye mtandao [4]). Zaidi ya kutoa habari za kawaida zinaihusu Uganda na kufuatilia maendeleo ya sehemu nne muhimu za mradi [5], mradi huo umekuwa ukiwafundisha wakazi wa sehemu hiyo jinsi ya kutumia kamera za video ili kusimulia maisha yao:

[Mnamo mwezi wa Pili], karibu ya watu 20 kutoka Katine walihudhuria warsha tatu za video zilizofanyika katika kituo cha habari, ambayo sasa imefunguliwa kwa ajili ya wanakijiji katika ofisi za AMREF kwenye kitongoji hicho.

Kamera nne za video na meza zake vimeachwa katika kituo hicho kwa ajili ya kuwaazima wanakijiji ili warekodi hadithi zao…

Madhumuni ya kituo hicho ni kuwapatia wanachama wa jumuiya ya Katine jukwaa la kuongelea maisha yao – changamoto na fursa, mawazo yao kuhusu kazi inayofanywa na Amref – na kuwapa njia ya kupata habari pamoja na utaalamu.

Video zinazotengenezwa huonyeshwa katika sehemu ya Sauti za Vijijini [6] za mradi huo. Katika moja ya video hizo, mkazi wa Katine John Ogalo anawaonyesha watazamaji kaya yake na anahudhuria misa kanisani. Video nyingine inamfuatilia mwendesha teksi Denis Ewalu [7]wakati akifanya ukarabati wa baiskeli yake, akijadili bei na wateja wake na kuendesha karibu kilometa 80 (maili 50) katika siku moja.

Sehemu ya Sauti za Vijijini pia inawaunganisha wasomaji na wakazi wa sehemu hiyo kwa kutumia ujumbe wa maandishi. Ujumbe mmojawapo unaelezea habari ya wanafunzi watatu wa kike [8] ambao wanajadili matumaini yao ya maisha ya baadaye.

Teresa Acupo
Huko mbeleni, ninataka kusoma siasa na kuwa mbunge wa eneo letu. Wabunge wanapata pesa nyingi sana na wanaheshimiwa.

Susan Amweso
Ndoto yang uni kuwa mwanamke huru kifedha. Ninataka kudhibiti pesa zangu mimi mwenyewe, na sio kumtegemea mume wangu kwa kila kitu.

Magdalene Atai
Babu na bibi yangu wamewajibika kunitunza wakati ninakua na nitakapomaliza masomo, niwanunulia zawadi kila mmoja. Na kwa sababu wanaweza wakashindwa kunisomesha mpaka chuo kikuu, ningependa kujifunza uuguzi baada ya kumaliza elimu ya sekondari. Hivyo ndivyo wanavyofanya wasichana wengi ambao hawana uwezo wa kujilipia elimu ya juu. Kadhalika ni rahisi kupata kazi kama muuguzi. Mtu yeyote anaweza kuanzisha zahanati binafsi kijijini ili kujikimu.

Wakazi 25, 000 wa Katine wanaishi nje ya maeneo yenye umeme. Bila ya mradi wa Katine, pengine watu hawa wasingeweza kuisimulia dunia hadithi zao.